Ghailani aondolewa mashtaka
18 Novemba 2010Jopo la majaji huko Marekani limemuondolea mashtaka kadhaa mshukiwa wa mashambulizi ya kigaidi katika balozi za Marekani nchini Kenya na Tanzania.
Ahmed Ghailani amepatikana na hatia ya shtaka moja tu la kushirikiana na watu waliozishambulia balozi hizo mbili za Marekani mwaka 1998, na kusababisha vifo vya watu 224, ikiwemo Wamerakani 12.
Waendesha mashtaka walisema wamefurahishwa na uamuzi huo wa jopo hilo la majaji, na kwamba Ghailani sasa anakabiliwa na kifungo kisichopungua miaka 20 jela vile vile uwezekano wa kifungo cha maisha kwa kuhusika kwake katika mashambulizi hayo.
Mwanasheria wa Marekani Preet Bharara alisema watapigania Ghailani afungwe maisha jela, pasi na kupewa msamaha wakati jopo hilo litakapokutana tena kuamua hukumu ya Ghailani Januari 25.