Gbagbo apuuza wito wa ECOWAS kung'atuka madarakani
29 Desemba 2010Hata hivyo,wajumbe kutoka Jumuiya ya Uchumi ya nchi za Afrika Magharibi, ECOWAS wanajaribu kumshwashi kiongozi huyo kubadili msimamo wake.Kwa wengi hiyo ni kazi ngumu, lakini hiyo wala haikuwavunja moyo marais wa Benin, Sierra Leone na Cape Verde. Kwani siku ya Jumanne viongozi hao walikwenda Abidjan kukutana na Gbagbo kwa azma ya kumshinikiza kung'átuka madarakani wakiwa na ujumbe uliotoka ECOWAS.
Lakini Gbagbo, anaeamini kuwa yeye ndie aliyeshinda uchaguzi wa rais, anaendelea kungángánia madaraka. Kwa hivyo, viongozi wa Afrika Magharibi wanashauriana juu ya hatua ya kuchukuliwa baada ya Gbagbo hiyo jana kupuuza wito wa kuondoka madarakani kwa hiyari au kukabiliwa na hatua za kijeshi. Hii leo marais hao watatu wanakutana na Rais wa Nigeria, Goodluck Jonathan, mjini Abuja, baada ya hiyo jana kuondoka Abidjan bila ya kufanikiwa. Wajumbe hao wa ECOWAS walitumaini kufuatana na Gbagbo uhamishoni.
Kwa upande mwingine, Gbagbo anasema kuwa yeye ni mhanga wa njama ya kimataifa inayoongozwa na Ufaransa. Azma anasema kuwa ni kumweka madarakani mpizani wake, Alassane Ouattara, anayeaminiwa na Ufaransa kinyume na Gbagbo. Ukweli ni kwamba kuhusu suala la Cote d’Ivoire, mkoloni wa zamani, Ufaransa, ilishika bendera.
Rais Nicolas Sarkozy alikuwa wa kwanza kumshinikiza Laurent Gbagbo kuondoka madarakani na hata kuweka vikwazo dhidi yake. Lakini nchini Ufaransa wapo pia wanaokosoa msimamo huo, na mmoja wao ni waziri wa zamani wa Ufaransa katika Umoja wa Ulaya, Pierre Moscovici aliesema:
"Ufaransa haipaswi kuwa mstari wa mbele katika mzozo huo. Kweli tuna maslahi nchini Cote d'Ivoire, tuna wanajeshi na raia wetu. Lakini si wajibu wetu kumshinikiza kiongozi wa nchi. Ninaamini kuwa ni wajibu wa Waafrika wenyewe kupata suluhusho la mzozo huo."
Na hivyo ndio itakavyokuwa ikiwa kutazuka vita vya wenyewe kwa wenyewe. Kwani Ufaransa imeshatamka kuwa haitoingilia kijeshi mzozo huo. Wanajeshi wake 900 waliopo Cote d’Ivoire wanapaswa kushughulikia tu usalama wa raia wake nchini humo.
Kwa hivyo, wajibu wa kulinda usalama wa raia wa Cote d’Ivoire utabakia mikononi mwa wanajeshi wa Umoja wa Mataifa wapatao kama 9,000. Vikosi hivyo vinaendelea kubakia Cote d’Ivoire licha ya kuamriwa na Gbagbo kuondoka nchini humo. Sasa yadhihirika kuwa mashambulio yanayolenga vikosi hivyo vya amani yanaongezeka. Hiyo jana, mlolongo wa magari ya vikosi hivyo vya Umoja wa Mataifa, ulishambuliwa na umati wa watu ukingoni mwa mji mkuu Abidjan. Mwanajeshi mmoja alijeruhiwa na gari moja liliteketezwa kwa moto katika shambulizi hilo.
Kwa kweli, uchaguzi wa mwezi uliopita ulikuwa na azma ya kumaliza mivutano iliyozuka kufuatia vita vya wenyewe kwa wenyewe vya mwaka 2002 . Lakini mgogoro huu mpya, umesababisha wasiwasi miongoni mwa raia wa Cote d’Ivoire na wamenza kuikimbia nchi hiyo. Kwa mujibu wa UNHCR -shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia wakimbizi, zaidi ya watu 19,000 wamekimbilia nchi jirani Liberia.
Mwandishi:Dugge,Marc/ZPR
Mpitiaji: Othman,Miraji