GAZA CITY : Mauaji ya watoto yalaaniwa
11 Desemba 2006Matangazo
Maelfu ya Wapalestina wameandamana huko Gaza baada ya watu wenye silaha wasiojulikana kuwauwa watoto watatu wa afisa mwandamizi wa ujasusi mfuasi wa kundi la Fatah la Rais Mahmoud Abbas.
Waandamanaji waliokuwa wamekasirika walilivamia eneo la jengo la bunge na kufyetuwa risasi wakati wa maandamano hayo. Mauaji hayo ya watoto hao wenye umri kati ya miaka sita na tisa yalitokea leo asubuhi wakati watoto hao walipokuwa wakiteremshwa kwenye gari kwenda shule katika mji wa Gaza.
Hakuna mtu aliyedai kuhusika na shambulio hilo na chama tawala cha Hamas kimelaani mauaji hayo.
Rais Mahmoud Abbas amelaani mauaji hayo kuwa ni mabaya na ni uhalifu uliokosa ubinaadamu uliotendwa na watu wasiothamini uhai.