1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Florian Wirtz bado yupo yupo sana Bayer Leverkusen

1 Machi 2024

Baba mzazi wa mchezaji Florian Wirtz, Hans Wirtz, amewatoa hofu mashabiki wa timu hiyo baada ya kuweka wazi kuwa kijana wake bado atasalia katika klabu hiyo hata baada ya msimu huu wa Bundesliga kukamilika.

https://p.dw.com/p/4d5Ez
Bundesliga I  Bayer Leverkusen | Florian Wirtz
Mchezaji wa Bayer Leverkusen Florian Wirtz anawindwa na vilabu vya Barcelona, real Madrid na Bayern Munich.Picha: Fabian Bimmer/REUTERS

"Florian ana mkataba Leverkusen hadi 2027. Kwa hivyo, huo ndio muda ambao tunaweza kusema ataitumikia Leverkusen," Hans Wirtz, ambaye pia ni meneja wa mchezaji huyo, aliyasema hayo wakati akizungumza na gazeti la Kölner Stadt-Anzeiger siku ya Ijumaa (Machi 1).

"Hakuna jibu la nini kitatokea baada ya hiyo miaka miwili iliyosalia lakini tusubiri njia itaelekea wapi." Alisema mzazi huyo.

Kiungo mshambuliaji Wirtz mwenye miaka 20, ni mmojawapo ya vipaji vikubwa sana vya Ujerumani na ameisaidia klabu yake ya Leverkusen kushinda michezo 33 katika mashindano yote huku wakiwa juu kileleni mwa ligi ya Ujerumani, Bundesliga, kwa tofauti ya alama 8.

Soma zaidi:Leverkusen waendelea kuwaumisha kichwa Bayern 

 

Kocha wa Wirtz naye atajwa

Michezol | Bundesliga | Bayer Leverkusen
Kocha mkuu wa Bayer Leverkusen, Xabi Alonso, akimpa maelekezo kiungo mshambuliaji wa timu hiyo, Florian Wirtz.Picha: Anke Waelischmiller/Sven Simon/picture alliance

Kwa upande mwingine tetesi za soka zinaonesha kuwa kocha wake, Xabi Alonso, ambaye amempa nafasi ya kung'ara nyota huyo, naye anahusishwa kujiunga na klabu zake za zamani za Bayern Munich na Liverpool, ambazo zinahitaji makocha wapya katika majira ya joto.

Mpaka sasa Wirtz amecheza mechi 14 za timu ya taifa ya Ujerumani, ingawa baba yake anaamini bado nyota huyo ana safari ndefu ya kufikia mafanikio.

Taarifa zilizoenea zinataja kuwa vilabu vya Bayern, Barcelona na Real Madrid vimeonesha nia ya kumtaka.