1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Congo yatolewa katika dimba la CHAN

Bruce Amani
21 Agosti 2017

Burkina Faso iliifunga Ghana mabao mawili kwa moja hapojana kwenye mchuano wa duru ya kufuzu katika dimba la Kombe la Mataifa ya Afrika kwa wachezaji wa ligi za ndani – CHAN.

https://p.dw.com/p/2iZk6
CHAN Cup African Nations Championship DRC Feier
Picha: DW/J. Kanyunyu

Mabingwa watetezi Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na timu waliyoifunga katika fainali ya 2016, Mali, walibanduliwa nje ya dimba hilo siku ya Jumamosi.

Ghana, makamu bingwa mara mbili katika awamu nne za mwisho za dimba hilo, ilitoka sare ya mabao mawili kwa mawili na Burkinabe katika mechi ya mkondo wa kwanza.

Hivyo Burkina Faso imefuzu kwa jumla ya mabao manne kwa matatu na itajiunga na nchi nyingine 15 katika dimba hilo linalochezwa kila baada ya miaka miwili, na ambalo litaandaliwa Kenya kuanzia Januari 12 hadi Februari 4.

Katika eneo la Afrika Mashariki, Uganda ilifuzu kwa jumla ya mabao matatu kwa mawili baada ya kuiangusha Rwanda licha ya kuzabwa mbili sifuri mjini Kigali katika mchuano wa marudiano.

Aidha Sudan ilifuzu baada ya kuiangusha Ethiopia kwa jumla ya bao moja kwa sifuri. Namibia ilijikatia tikiti kwa mara ya kwanza baada ya kuwafunga Wacomoro mabao mawili kwa bila. Kenya na Guinea ya Ikweta, ambao walifuzu baada ya Gabon kujiondoa, pia watashiriki dimba hilo la CHAN kwa mara ya kwanza.

Mwandishi: Bruce Amani/Reuters/AFP
Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman