1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Chelsea washeherekea, Bayern wahuzunika

21 Mei 2012

Chelsea, baada ya kushinda kombe la Mabingwa Ulaya, dhidi ya Bayern Munich walikaribishwa kwa shangwe na mashabiki wao mjini London. Mjini Munich, nahodha wa Bayern Philip Lahm alisema timu yake itafufuka tena

https://p.dw.com/p/14zUm
Chelsea players celebrate with their Champions League trophy during a parade in London, Sunday, May 20, 2012. Chelsea's Didier Drogba scored the decisive penalty in the shootout as Chelsea beat Bayern Munich to win the Champions League final in Munich, Germany after a dramatic 1-1 draw on Saturday, May 19. (Foto:Lefteris Pitarakis/AP/dapd).
Champions League Pokal Chelsea feiert in LondonPicha: AP

Maelfu ya mashabiki wa Chelsea waliwakaribisha mashujaa wao nyumbani hapo jana jioni wakati timu hiyo ilipoandaa msafara katika barabara za magharibi mwa London ambako ni nyumbani kwa mabingwa hao wapya wa Ulaya. Wachezaji wa Chelsea pamoja na mmiliki wa klabu hiyo Roman Abramovich walikuwa juu ya basi la wazi ambako waliwaonyesha mashabiki wao kombe la Bara Ulaya na lile la FA. Chelsea waliwadiwaza Bayern Munich katika uwanja wao wa Allianz Arena mjini Munich Ujerumani, kwa kuwafunga magoli manne kwa matatu kupitia mikwaju ya penalti baada ya mchezo kumalizika sare ya bao moja kwa moja katika muda wa kawaida na wa ziada.

Hiyo ndiyo mara ya kwanza kwa Chelsea kushinda kombe hilo la Ulaya na kutimiza ndoto ya mmiliki wa klabu hiyo Mrusi Roman Abramovich ambaye amewekeza mamilioni ya pauni katika klabu hiyo.

Cameron ashangilia
Lakini wakati takriban watazajai milioni 300 wakifuatilia matukio hayo moja kwa moja kote ulimwenguni, kutoka uwanja wa Allianz Arena, kulikuwa na mashabiki wengine ambao hawakutaka kupitwa na tukio hilo. Waziri Mkuu wa Uingereza David Caremon aliushangilia ushindi wa Chelsea hapo jana baada y akuiangalia penalty ya ushindi akiwa pamoja na Kansela Angela Merkel katika mkutano wa kilele wan chi tajiri zaidi ulimwenguni G8 nchini Marekani.

Merkel haonekani kuwa na furaha kutokana na kile anachotazama
Merkel haonekani kuwa na furaha kutokana na kile anachotazamaPicha: Reuters

Cameron aliwaambia waandishi habari mjini Chicago kabla ya mkutano wa G8 kuwa siyo kila mara unapata fursa ya kuangalia awali ya kupiga mikwaju ya penalti kati ya timu ya Uingereza na timu ya Ujerumani na uangalie timu ya Uingereza ikishinda.

Cameron alipigwa picha akiwa amenyanyua juu mikono akishangilia fainali hiyo ya Jumamos kupitia televisheni akiwa pamoja na viongozi wengine wa ulimwengu akiwemo rais Barack Obama na Angela Merkel.

Hii ilikuwa ni kama kulipiza kisasi kwa Cameron baada ya yeye na Merkel kuangalia mchuano ambao Ujerumani ilizaba Uingereza mabao manne kwa moja katika mechi ya kombe la dunia mwaka 2010. wawili hao waliangalia mchuano huo kupitia televisheni wakati wa mkutano wa kilele wa G20 mjini Toronto, Canada.

Kukadiria hasara mjini Munich
Mjini Munich, Mkurugenzi wa Spori wa Bayern Munich Christain Nerlinger alisema kichapo cha Jumamosi katika uwanja wao wa nyumbani hakikuwa kitu cha kutuma katika kaburi la sahau kwa usiku mmoja. Nerlienger alisema ni kichapo kitakachowaandama kwa sababu tulikosa nafasi ya kihistoria. Rais wa Bayern Uli Hoeness aliitaja fursa ya Bayern ya kupata nafasi za kona 20 wakati wa fainali hiyo akisema hawezi kukubali kuwa wa pili kila mara. Katika msimu wa Bundesliga uliokamilika hivi majuzi, Bayern ilimaliza katika nafasi ya pili nyuma ya mabingwa wa 2012 Borussia Dortmund.

Bastian Schweinsteiger haamini kuwa alipoteza mkwaju wa penalti
Bastian Schweinsteiger haamini kuwa alipoteza mkwaju wa penaltiPicha: Reuters

Mwenyekiti wa Bayern Karl-Heinz Rummenigge alisema kichapo cha Jumamosi kilikuwa kibaya hata zaidi kuliko kile cha mwaka wa 1999 waliposhindwa na Manchester United katika fainali ya mwaka huo ya Ligi ya Mabingwa mjini Barcelona.

Nahodha Philip Lahm alisema kushindwa huko kutawapa fursa ya kurejea tena kwa kishindo. Alisema wangali katika umri mzuri na sasa wana njaa hata zaidi ya kupata mataji.

Kocha wa Ujerumani atathimini

Akizungumza katika kambi ya maozezi ya timu ya taifa mjini Tourrettes kusini mwa Ufaransa, kocha Joachim Loew alisema wachezaji wa Bayern baada ya siku chache watajinyanyua na kusahahu yaliyopita. Alisema walifika fainali na walikuwa timu bora. Na kwamba hakuna haja ya wao kushuku ubora wao.

Wachezaji wanane wa Bayern wanaochezea timu ya taifa ya Ujerumani wanajiunga na kikosi cha mwanzo cha Loew cha wachezaji 27 baadaye wiki hii huku Ujerumani ikijiandaa kwa dimba la mataifa ya ulaya maarufu kama euro 2012 litakaloandaliwa nchini Poland na Ukraine kuanzia tarehe nane Juni.

Mwandishi: Bruce Amani
Mhariri: Yusuf Saumu