1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Catalonia kuendelea na kura ya maoni ya tarehe mosi, Oktoba

Zainab Aziz
29 Septemba 2017

Zimebaki siku mbili kabla ya kura ya kutaka uhuru wa jimbo la Catalonia. Hatua hiyo inapingwa vikali na serikai ya Uhispania lakini viongozi wa eneo hilo leo wamesisitiza kuwa hakuna litakalowazuia.

https://p.dw.com/p/2kzRC
PK der katalanischen Regierung in Barcelona
Picha: Reuters/J. Medina

Viongozi wanaosimamia mchakato wa kutafuta uhuru wa Catalonia wameahidi kuendelea na zoezi la kupiga kura ya maoni katika eneo hilo lenye watu milioni 7.5 licha ya pingamizi kutoka kwenye serikali ya Uhispania. Kiongozi wa jimbo hilo Carles Puigdemont amesema ana imani kubwa kwamba wapiga kura watazingatia Amani siku ya kupiga kura ambayo ni tarehe 1.10. Kiongozi huyo amewatolea wito polisi wa Uhispania ambao anasema wamepelekwa kwa wingi katika jimbo la Catalonia kwamba wasijaribu kuwazuia watu wa jimbo lake kushiriki katika zoezi la kupiga kura hiyo ya maoni. Puigemont amewaomba polisi kuzingatia utalaam wa kazi yao kuliko kuegemea upande wa kisiasa.

Wakulima, wazima moto na kikosi cha polisi cha kanda ya Catalonia Mossos d'Esquadra,wameapa kulinda vituo vya kupigia kurana pia wamewaonya polisi wa Uhispania juu ya hatari zinazoweza kutokea iwapo watajaribu kuvuruga utaratibu wa umma au kuwazuia watu kupiga kura. Lakini wizara ya mambo ya ndani ya Uhispania, ambayo jukumu la usalama had katika siku hiyo ya kupiga kura, inasisitiza kuwa polisi wa catalonia wanapaswa kuchukua hatua na iwapo watakataa basi serikali imeshatuma maelfu ya maafisa wa ziada kutoka Madrid ili kuhakikisha kuwa kura hiyo haifanyiki kwa sababu sio halali.

Spanien Madrid Premierminister Rajoy Rede zu Referendum Kataloniens
Waziri mkuu wa Uhuspania Mariano RajoyPicha: Getty Images/AFP/J. Soriano

Serikali ya Uhispania imehimiza kuachiliwa mbali kura hiyo ya maoni  baada ya hapo baada ya uhalali wake kubatilishwa na Mahakama ya Katiba. Polisi wamewakamata baadhi ya viongozi wa wanaounga mkono uhuru wa Catalonia na pia wametwaa mamilioni ya karatasi za kupigia kura. Kiongozi mmoja wa jimbo la Catalonia Oriol Junqueras amewaambia waandishi wa habari mjini Barcelonakwamba hatua zinazochukuliwa na serikali ya Uhispania kwa lengo la kuvuruga au kuharibu kura hiyo ya maoni hazitawadhoofisha watu wa Catalonia bali zitazidi kuwaimarisha na kwamba wao wanafanya kila kinachowezekana kuwawezesha raia wote kupiga kura.

Polisi wameagizwa kuweka doria kweyne shule, ambazo zitatumika kama vituo vya kupigia kura. Junqueras amesema zaidi ya watu milioni 5.3 wa jimbo la Catalonia wanatarajiwa kupiga kura katika jumla ya vituo 2,315 kuanzia saa moja asubuhi hadi  saa kumi na mbili jioni. Junqueras amefahamisha kwamba wanatarajia kutangaza uhuru wa eneo lao ndani ya saa 48 ikiwa Wacatalan wataipa ushindi kuwra ya 'ndiyo' kama inavyotarajiwa hata ingawa Wacatalonia wanaopendelea kubakia kwenye Uhispania moja huenda wasishiriki katia kura hiyo ya maoni itakayofanyika wiki ijayo.

Mwandishi: Zainab Aziz/AFPE/DPAE

Mhariri: Yusuf Saumu