Burkina Faso yafanya uchaguzi wa rais
22 Novemba 2010Wananchi wa Burkina Faso wamepiga kura katika awamu ya kwanza kumchagua rais wa nchi hiyo ya Afrika ya Magharibi, ambapo kiongozi aliyeko madarakani, Blaise Compaore, anatarajiwa kupita tena bila ya wasiwasi.
Compaore alietwaa mamlaka mnamo mwaka wa 1987 nchini Burkina Faso anawania muhula wa nne wa urais baada ya kushinda katika chaguzi tatu zilizopita.
Katika uchaguzi wa mwaka 2005 kiongozi huyo alizoa asilimia zaidi ya 80 ya kura. Watu milioni 3 na laki mbili waliojiandikisha wanawapigia kura pia wagombea wengine sita wanaoviwakilisha vyama vya kisiasa vilivyomegekamegeka.Ishara zote zinaonyesha kwamba Compaore atashinda na kukitumikia kipindi cha nne.
Hata hivyo uchaguzi huo haukuivutia sana jumuiya ya kimataifa kutokana na migogoro ya uchaguzi iliyozikabili nchi jirani za Ivory Coast na Guinea.
Wakati huo huo Compaore anasuluhisha katika mgogoro wa Guinea ambapo watu wasiopungua10 walikufa kutokana na ghasia zilizofuatia uchaguzi.