1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bundesliga kuanza rasmi Ijumaa

Sekione Kitojo
14 Agosti 2017

Bundesliga kuanza kutimua vumbi Ijumaa hii, wakati katika kombe la shirikisho la Ujerumani DFB Pokal, timu kadhaa za ligi daraja la kwanza zanusurika

https://p.dw.com/p/2iCqH
Fußballstadien in Deutschland- Allianz Arena in München
Picha: picture-alliance/SvenSimon

Bundesliga inaanza  kutimua  vumbi  siku  ya  Ijumaa tarehe  18  kwa  pambano  kati  ya  mabingwa  watetezi Bayern  Munich  na  Bayer  Leverkusen  katika  uwanja  wa Allianz  Arena. Lakini  nini  kinachotarajiwa  mara  hii  katika msimu  huu  wa  55  wa  Bundesliga, ambapo  timu zinazoonekana  kuwa  na  utamaduni  wa  kushika  nafasi za  juu  kama  Schalke 04, Bayer Leverkusen , Borussia Moenchengladbach  zimeporomoka  na  hata  hazimo katika  mashindano  ya  ligi  ya  Europa, mara  hii.

Fußball Bundesliga Ousmane Dembele FC Schalke 04 - Borussia Dortmund
Ousmane Dembele wa Borussia Dortmund anataka kuhamia FC BarcelonaPicha: picture-alliance/Sport Moments/Paschertz

Kwa  upande  wa  tetesi  za  kuhama  wachezaji , tetesi kumhusu Ousmane  Dembele  wa  Borussia  Dortmund hazija muacha  salama. Kila  siku  tetsi  hizo  zinazidi kuongezeka  akihusishwa  na  kuhamia  FC  Barcelona  ya Uhispania.  Dembele  kutokana  na  utovu  wa  nidhamu ambapo  alishindwa  kufika  katika  mazowezi  ya  timu hiyo  siku  ya  Alhamis ameadhibiwa  kwa  kuondolewa katika  kikosi  cha  kwanza  na  atakaa  nje  ya  kikosi  hicho hadi  mwishoni  mwa  mwezi  huu.

Dembele  amefanya hivyo  akitaka  kutoa  mbinyo  kwa  timu  yake  kumruhusu kwenda  kuchezea  Barcelona. Barcelona  wametoa  kiasi cha  euro milioni 90  pamoja  na  malipo  mengine  ya bonasi  hapo  baadae  kuweza  kumpata  mchezaji  huyo chipukizi  mwenye umri  wa  miaka  20, raia  wa  Ufaransa. Lakini  Dortmund  wamekataa  wakitaka  kitita  cha  euro milioni 140  hadi 150  ili  kuweza  kumuachia  mchezaji huyo.

Rot-Weiss Essen v. Borussia Dortmund Ousmane Dembele
Mchezaji wa kiungo wa Borussia Dortmund Ousmane DembelePicha: Bongarts/Getty Images

Barcelona yatakiwa kusajili wachezaji wapya

Barcelona inalazimika  kusajili  wachezaji  wapya , amesema  mchezaji  wa  kiungo  wa  timu  hiyo Sergio Busquets , na  timu  hiyo  inawania  kuwasajili  Ousmane Dembele  wa  Borussia  Dortmund  na Philippe Coutinho wa  Liverpool  ili  kuimarisha  kikosi  chake  kilichoondokewa na  mchezaji  nyota  Neymar  ambaye  ametimkia Paris St. Germain  kwa  kitita  cha  milioni  222.

Baada  ya Barcelona  kutwanga  mabao 3-1  na  mahasimu  wao wakubwa  Real Madrid jana  Jumapili  katika  kombe  la Super Cup , linaloashiria  kufungua  msimu  wa  ligi  ya Uhispania , tayari  imechukua  hatua  ya  kukiimarisha kikosi  chake  na  wamepata  saini  ya  mchezaji  wa kiungo Paulinho  kutoka  klabu  ya Guangzhou Evergrande kwa  kitita  cha  euro  milioni 40 , klabu  hiyo  imethibitisha leo.

Fußball - Spanischer Super Cup - FC Barcelona gegen Real Madrid
Cristiano Ronaldo afungiwa michezo mitano kwa kumsukuma mwamuzi baada ya mchezo wa Super Cup dhidi ya BarcelonaPicha: picture alliance/Zumapress/M. Blondeau

Barcelona  inaelekea  mjini  Madrid  kupambana  na  Real Madrid  katika  mkondo  wa  pili  wa  kinyang'anyiro  cha kombe  la  Super Cup  huku  ikiwa  na  matumaini  finyu  ya kuweza  kurejesha  mabao  hayo, licha  ya  kuwa mshambuliaji  hatari  wa  Real Madrid Cristiano  Ronaldo hatakuwamo  katika  kikosi  hicho  kutokana  na  kupewa kadi  nyekundi  katika  mchezo  huo. Hata  hivyo  kocha  wa Real Zinedine Zidane  amesema  klabu  yake  itafikiria kukata  rufaa  kwa  uamuzi  huo  katika  shirikisho  la kandanda  la  Uhispania kupinga  kadi  ya  pili  ya  njano dhidi  ya  Ronaldo.

TSG Hoffenheim yaikabili Liverpool

TSG  Hoffenheim  ya  Ujerumani  inakutana  na  FC Liverpool  ya  Uingereza  katika  mkondo  wa  kwanza  wa mchezo  wa  mchujo  wa  kuwania  kufika  katika  awamu ya  makundi  ya  Champions League  barani  Ulaya , na kufikia kilele  cha  safari  yao inayoonesha  mafanikio makubwa  kwa  timu  hiyo  ya  kijijini  Sinsheim , nchini Ujerumani. Hoffenheim  na  Liverpool  zina  historia  tofauti kabisa  na vigogo  hao  barani  Ulaya wako  katika  historia tofauti  kabisa  wakati  wakiingia  katika  awamu  hii  ya mchujo  ya  kombe  hilo.

Liverpool ni  mabingwa mara  tano  wa  kombe  hilo  wakati Hoffenheim  ndio  kwanza  wanaonja  mikiki mikiki  ya kinyang'anyiro  hicho, baada  ya  kumaliza katika  nafasi  ya nne  katika  Bundesliga  msimu  uliopita.

Lakini  katika  kikosi  cha  kocha  Jurgen Klopp  wa Liverpool  mchezaji  mmoja  anakosekana. Philippe Coutinho  ameachwa  nyumbani , bila  shaka  kutokana  na majadiliano ya  kutaka  kujiunga  na  Barcelona  ya Uhispania.

 

Mwandishi: Sekione  Kitojo  / afpe /dpae / ape / rtre

Mhariri: Mohammed Khelef