1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

BERLIN:Uingereza yazidisha shinikizo kutaka wanamaji wake waachiwe

26 Machi 2007
https://p.dw.com/p/CCFK

Waziri Mkuu wa Uingereza Tony Blair amesema kushikiliwa kwa askari 15 wa majini na Iran hapo siku Ijumaa ni kinyume cha sheria na ni makosa.

Uingereza mpaka sasa haijapewa fursa iliyoomba ya kujua walipo wanamaji hao.

Iran imesema kuwa wanamaji hao walikamatwa baada ya kuingia katika eneo la bahari ya Iran,bila ruhusa lakini Uingereza imesisitiza kuwa walikuwa katika doria ya kawaida.

Uingereza na Ujerumani ambayo kwa sasa ndiyo rais wa Umoja wa Ulaya zote zimetaka kuachiwa mara moja kwa wanamaji hao.

Wakati huo huo Rais Hugo Chavez wa Venezuela ametoa wito kwa mataifa duniani kuzuia kile alichokiita mipango ya Marekani kuishambulia Iran.

Akizungumza hapo jana siku moja baada ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kupiga kura ya kuzidisha vikwazo dhidi ya Iran kufuatia nchi hiyo kukataa kusitisha mpango wake wa nuklia, Chavez amesema kuwa Marekani imekuwa ikisogeza majeshi yake karibu na Iran.

Chavez alinukuu taarifa zilizotolewa na vyombo vya habari vya Urusi, ambazo zilieleza kwa kina, muda na wapi shambulizi hilo litafanyika.

Amesema kuwa ana matumaini bunge la Congress la Marekani,Umoja wa Mataifa na mataifa mengine yenye nguvu yatazuia kile alichikiita wendawazimu wa taifa la Marekani kushambulia yoyote asiyokubaliana naye.

Kiongozi huyo wa Venezuela ni swahiba mkubwa wa Rais Fidel Castro wa Cuba na hasimu mkubwa wa Rais George Bush wa Marekani.

Mjini Tehran, serikali ya Iran imetangaza kupunguza uhusiano na shirika la nguvu za Nuklia la Umoja wa Mataifa.

Msemaji wa Serikali ya Iran pia amesema kuwa nchi hiyo itaendelea na mpango wake wa kuzalisha nishati ya nuklia.