Bayern na mtihani mkubwa dhidi ya Porto
20 Aprili 2015Timu ya Guardiola iliyovurugika kutokana na majeruhi chungu nzima ililazwa magoli matatu kwa moja na Porto katika mkondo wa kwanza wa robo fainali. Kicha daktari wa timu, Hans-Wilhelm Mueller-Wohlfahrt, akafungasha virago baada ya karibu miongo minne katika klabu hiyo, akisema yeye na kikosi chake wamelaumiwa kwa njia isiyo halali kufuatia kichapo cha Porto. Hayo yanajiri wakati Pep Guardiola akipuuzilia mbali madai kuwa anapanga kuondoka katika klabu ya Bayern. "Naijua timu ninayoiongoza na najua kuwa ubingwa wa ligi na klabu bingwa ulimwenguni havitoshi. Hii ni Bayern Munich, kama Barcelona, kama Real Madrid, kama vilabu vikubwa ulimwenguni. katika hali hii, ni mataji matatu pekee yatakayotosha. Katika miezi ya nyuma, kawaida niliamua kuhusu timu yangu ya kwanza saa moja kabla ya mpambano. Lakini katika hali ya sasa, bado sijui nini kitafanyika kesho".
Nahodha Philipp Lahm amesema wamejipanga sawasawa na wataitumia faida ya kucheza mbele ya mashabiki wa nyumbani "Nafasi yetu ya mwanzo siyo nzuri lakini siyo kwamba haiwezekani. Hivyo ndivyo tunapaswa kuungalia mpambano huo. Tuna kila fursa. Tutacheza nyumbani mbele ya mashabiki wetu ambao watatushangilia hadi mwisho. Tunapaswa kuwa makini kuanzia mwanzo na kujaribu kufunga goli la mapema. Kisha kila kitu kitawezekana. Robo fainali ya Ligi ya Mabingwa ni ya kusisimua. Tunataka kufuzu katika nusu fainali".
Bastian Scheinsteiger alifamya mazoezi jana na ataweza kurejea wakati Franck Ribery na nahodha Philip Lahm wakitiliwa mashaka. Bila shaka Guardiola atakosa huduma za Arjen Robben, David Alaba, Mehdi Benatia, Javi Martinez na mlinda mlango wa akiba Tom Starke.
Nao Barcelona ina mguu mmoja katika nusu fainali kufuatia ushindi wa ugenini wa mabao matatu kwa moja dhidi ya Paris Saint-Germain kabla ya mchuano wao wa kesho wa marudiano.
Mabingwa watetezi Real Madrdi watapambana na adui ambaye wanamfahamu vyema Atletico Madrid ili kujikatia tikiti ya kucheza nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya. Watani hao wa mji wa Madrid walitoka sare ya bila kufungana katika mkondo wa kwanza wa robo fainali, na hivyo basi kutakuwa na kibarua kikali sana uwanjani Santiago Bernabeu siku ya Jumatano.
Pia siku hiyo ya Jumatano, Monaco wanahitaji kuweka kando masaibu yao ya ligi ya nyumbani wakati watakapowakaribisha Juventus, baada ya kulambishwa goli moja kwa sifuri mjini Turin.
Mwandishi: Bruce Amani/AFP/DPA/Reuters
Mhariri: Yusuf Saumu