1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bakteria wa Ecolay wajulikana wametokea wapi

6 Juni 2011

Kishindo cha bakteria wa Ecolay,uamuzi wa kuachana na nishati ya kinuklea na kumalizika mkutano mkuu wa kanisa la kiinjili ndizo mada kuu magazetini

https://p.dw.com/p/11V9h
Bakteria wa Ecolay wachunguzwa katika maabara ya vyakula huko RostockPicha: picture alliance/dpa

Tuelekee kaskazini mwa Ujerumani ambako gazeti la "Nordseezeitung la mjini Bremerhaven linaandika kuhusu kishindo kilichosababishwa na bakteria wa Ecolay.

"Waziri wa kilimo wa jimbo la LowerSaxony,Gerd Linderman anastahiki kushukuriwa kutokana na moyo wa ujasiri aliokuwa nao jana usiku alipokutana na waandishi habari ili kuelezea haraka hali namna ilivyo,badala ya kuzidisha wahka miongoni mwa jamii.Hata kama bado hajapatiwa maelezo yote,lakini amefanikiwa kubainisha kwa uwazi kabisa ,nini chanzo cha bakteria wa Ecolay.Na kusema kweli hilo ndilo la muhimu zaidi,ufafanuzi ziada unaweza kutolewa siku zijazo."


Gazeti la Badische Neueste Nachrichsten la mjini Karlsruhe linahisi:

Hakuna jamii yoyote inayoweza kuepukana moja kwa moja na hatari inayoweza kupatikana ndani ya chakula.Inaweza kupatikana wakati wa kutengenezwa,kinapohifadhiwa katika ghala na pia wakati wa kukigawa pia.Hata hivyo kwa mara nyengine tena kisa cha bakteria wa Ecolay kinatutanabahisha juu ya umuhimu wa kununua kile kinachotokea nyumbani:Au kwa maneno mengine, mtu awe akiangalia kila wakati anachotaka kununua kinatokea wapi.Vyakula vinavyosafirishwa muda mrefu viepukwe.Na watu wasijali sana bei,ikiwa wanataka kuhifadhi afya yao."

Dossierbild Atomausstieg 3
Maandamano dhidi ya nishati ya kinukleaPicha: picture alliance/rtn - radio tele nord


Mada yetu ya pili magazetini inahusu uamuzi wa kuachana na nishati ya kinuklea.Gazeti la Hannoversche Allgemeine Zeitung linaandika:

Upande wa upinzani utasema nini?Ndo kusema wapakate mikono?Au wahoji uamuzi huo ni hafifu na umekawia kupitishwa?Wakati umewadia wa kuidaka fursa ya kihistoria iliyojitokeza .Mswaada wa sheria wa kuachana na nishati ya kinuklea ulioamuliwa na kansela Angela Merkel unawapatia wanasiasa muongozo wa aina mpya.Mkondo kama huo wa mageuzi ulijitokeza March 14 mwaka 2003 pale kansela wa zamani Gerhard Schröder alipotangaza mageuzi katika sekta ya ajira.Katika hali kama hiyo taifa zima hushirikiana.Haitoshi kuiachia serikali kunyosha mkono,na upande wa upinzani pia unawajibika kuchangia.

33. Deutscher Evangelischer Kirchentag in Dresden
Waumini katika mkutano mkuu wa kanisa la kiinjili mjini DresdenPicha: dapd


Mada yetu ya mwisho inahusu kumalizika mkutano mkuu wa kanisa la kiinjili.Gazeti la Westdeutsche Zeitung linaandika:

Kanisa limefanikiwa pakubwa mjini Dresden kubainisha msimamo wake katika masuala tofauti.Kwa namna hiyo imeelezwa wazi kabisa kwamba kujiingiza kanisa katika mijadala ya jamii sio tuu ni haki yake bali pia ni waajib wake.

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/Inlandspresse

Mhariri:Abdul-Rahman