1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Al Shabab wahujumu kituo cha AMISOM mjini Mogadischu

Oumilkher Hamidou17 Septemba 2009

Wanajeshi tisaa wa Umoja wa Afrika wauwawa na wengine kadhaa kujeruhiwa mjini Mogadischu

https://p.dw.com/p/JiuM
Wanamgambo wa kiislam wapiga doria MogadischuPicha: AP

Waasi wa kisomalia wameyaripua magari mawili yaliyosheheni mabomu katika kituo cha vikosi vya kulinda amani vya Umoja wa Afrika-AMISOM mjini Mogadischu-kwa kile ambacho waasi wanadai ni kisasi kwa kuuliwa wiki hii mwanaharakati wa ngazi ya juu wa mtandao wa kigaidi Al Qaida karibu na Barawa.

Ripota wa shirika la habari la Reuters amewaona wanajeshi sita waliojeruhiwa wakitolewa nje ya kambi hiyo,baadhi yao wamejeruhiwa vibaya sana huku moshi ukitanda angani katika mji mkuu huyo wa Somalia Mogadischu.

Duru za kuaminika zinasema wanajeshi tisaa wameuwawa.

Mashahidi wanasema magari mawili yaliyokua na kitambulisho cha umoja wa mataifa yaliingia katika kituo cha jeshi karibu na uwanja wa ndege,walikopiga kambi wanajeshi 5000 wa kikosi cha AMISOM.

Magari hayo yameripuka katika eneo ambako wanajeshi wa Amisom wanawapatia huduma za afya raia wa kawaida wa Somalia.

Kikosi hicho cha kusimamia amani kina wanajeshi wa kutoka Burundi na Uganda.

Msemaji wa jeshi la Uganda luteni kanali Felix Kulayigye akihojiwa na shirika la habari la Ufaransa AFP amesema mkuu wa vikosi vya kulinda amani,jenerali Nathan Mugisha wa kutoka Uganda amejerihiwa.

Muakilishi maalum wa Umoja wa Afrika nchini Somalia ,Nicolas Bwakira amethibitisha habari hizo na kulaani vikali mashambulio hayo aliyoyataja kua ni ya "kinyama."

Shahidi mmoja, Ali Mohamed ambae binafsi alikua akitibiwa katika kituo hicho anasema ameona maiti za watu wawili anaosema pengine ni wasomali.

Shambulio hilo linatajikana kua kubwa kabisa kuwahi kutokea dhidi ya vikosi vya kulinda amani vya Umoja wa Afrika tangu wanajeshi 11 wa Burundi walipouliwa na wengine 15 kujeruhiwa,mwezi February mwaka huu.

Karte Somalia Spanisch
Ramani ya SomaliaPicha: AP Graphics/DW

Msemaji wa wanamgambo wa itikadi kali ya dini ya kiislam,Al Shabab,Sheikh Ali Mahamud Rage amesema shambulio la leo limelengwa kulipiza kisasi kwa kuuliwa na vikosi maalum vya kimarekani Salah Ali Saleh Nabhan,jumatatu iliyopita kusini mwa Somalia.

Akitangaza habari hizo,Sheikh Ali Mahmoud Rage ameliambia shirika la habari la Reuters wamepata habari kwamba serikali ya Somalia na vikosi vya Umoja wa Afrika vinapanga kuwahujumu baada ya mwezi mtukufu wa Ramadhan .

Shambulio hilo limetokea pia saa chache baada ya Al Shabab kutoa masharti ya kumuachia huru mshauri wa masuala ya usalama wa Ufaransa wanaemshikilia mateka.

Masharti hayo ni pamoja na kuitaka Ufaransa iache kuisadia serikali ya Somalia na iwaondowe washauri wake wote wa masuala ya usalama kutoka somalia.

Waaasi wanataka wanajeshi wa Umoja wa Afrika wanaounga mkono utawala wa rais Sheikh Shariff Ahmed waihame nchi hiyo na manuari za kijeshi za Ufaransa zinazowaandama maharamia wa kisomali zirejee nyumbani.

Wanamgambo wa kiiislam wa Al Shabab wanadai pia wanaharakati wao wanaoshikiliwa katika nchi ambazo hazikutajwa,waachiwe huru.

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/Reuters&AFP

Mhariri:M.Abdul-Rahman