1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Al Shabaab wawakata shingo Wakenya 4

Sekione Kitojo
6 Septemba 2017

Polisi nchini Kenya wanasema raia waiopungua wanne wameuawa kwa kukatwa shingo na watu wanaoshukiwa kuwa wapiganaji wa kundi la al Shabaab lenye makao yake katika nchi jirani ya Somalia.

https://p.dw.com/p/2jQzk
Somalia Al-Shabaab Kämpfer
Picha: picture alliance/AP Photo/F. A. Warsameh

Mkuu wa polisi wa Pwani ya Kenya, Larry Krieng, amesema shambulio hilo lilifanyika siku ya Jumatano (Septemba 6) asubuhi katika eneo la Bobo, kijiji cha Hindi, Kaunti ya Lamu.

Shambulio hilo linapelekea idadi ya watu walioripotiwa kuuawa kwa kukatwa shingo na wafuasi wa al Shabaab katika Kaunti hiyo kuwa 16 katika kipindi cha miezi mitatu iliyopita.

Mauaji ya kukatwa shingo yalikuwa jambo la nadra nchini Kenya lakini ni ya kawaida nchini Somalia, ambako wafuasi hao wa itikadi kali wanayatumia kueneza hofu miongoni mwa wakaazi.

Al Shabaab imeapa kuiadhibu Kenya kwa hatua yake ya kutuma vikosi nchini Somalia kupambana na kundi hilo.

Kundi hilo limefanya mashambulizi kadhaa nchini Kenya tangu mwaka 2011, lakini mashambulizi ya karibuni yamejikita zaidi katika kaunti zinazopakana na Somalia.