AL AHLY ni washindwa wa Super Cup Afrika
19 Februari 2007Nüremberg jana ilinyemelea hadi pointi 1 mabingwa bayern Munich na sasa inatamani nafasi katika changamoto za msimu ujao za champions League-kombe la klabu bingwa barani Ulaya.Nüremberg iliilaza jana Energie Cottbus kwa bao 1:0.
Mabingwa Bayern Munich waliteleza tena mwishoni mwa wiki walipolazwa bao 1:0 na Alemania Aachen na sasa imeangukia nafasi ya 4 katika ngazi ya Bundesliga.
Viongozi wa Ligi Schalke nusra watoroke na pointi 3 lakini Wolfsburg dakika za mwisho iliizima Schalke na kuondoka nayo suluhu mabao 2:2.Sasa Schalke ina pointi 49-pointi 5 mbele kuliko Stuttgart walioizaba Eintracht Frankfurt mabao 4-0.
Bremen iliongoza Ligi hii kwa muda mrefu ilikiona jumamosi “kile kilichomtoa kanga manyoya”.Ilizabwa mabao 2:0 na majirani zao Hamburg.
Kesho “asie na mwana aeleke jiwe na asie na mguu atie gongo”-mkutano viwanjani katika champions league-kombe la klabu bingwa barani Ulaya:Mabingwa 7 wa zamani wataingia uwanjani kuania taji la msimu huu:
Bayern Munich kesho itabidi ijikaze kweli isiteleze tena itakapoumana na Real Madrid ya Spain kukata tiketi ya robo finali ya changamoto hii.
David Beckham atakuwa usoni upande wa Real Madrid baada ya kutengana na Ronaldo.Timu nyengine mabingwa wa zamani zitakazokuwa uwanjani ni pamoja na Manchester united na AC Milan.
Liverpool itaumana na FC Barcelona-mabingwa wa Ulaya wanaocheza tena majogoo wao wawili-Ronaldinho na Samuel Eto’o
Katika kombe la FA nchini Uingereza, Chelsea,mabingwa Tottenham Hotspurs,Manchester ,Watford na Playmouth Argyle zimeingia robo-finali.
Mabingwa wa Afrika al Ahly ya Misri jana waliongeza taji jengine katika kabati lao la vikombe kwa kushinda Kombe la Afrika la Super Cup. waliitoa nje Etoile du Sahel (Tunisia) mjini Addis Ababa kwa mabao 5-4 kufuatia changamoto za mikwaju ya penalty .
Hadi dakika ya 120 timu hizo mbili zilisimama sare 0:0.Kipa wa al Ahly Essam Al Hadari alionesha ushujaa wake kama katika finali ya mwaka jana na kuokoa mkwaju wa adhabu wa Khaled Melliti na hivyo kuipa ushindi Al Ahly.
Kombe la Afrika la “Super Cup” huaniwa nyumbani mwa mabingwa wa klabu bingwa lakini mara hii, lilihamishiwa Addis Ababa kama sehemu ya sherehe za kuadhimisha mwaka wa 50 tangu kuasisiwa kwa CAF-shirikisho la dimba la Afrika.
CAF inaadhimisha nusu karne ya dimba la Afrika katika nchi 4 zilizoasisi shirikisho hilo-Misri,Ethiopia,Sudan na Afrika Kusini.CAF iliundwa 1957.
Mkenya Danile Njenga jana aliwika katika Tokyo marathon alipochukua ushindi wake wa pili mnamo muda wa miaka 3 .Kijana huyo mwenye umri wa miaka 30 alichukua muda wa masaa 2:09.45 sek kumpiku alietazamiwa kushinda- Sammy Korir, pia kutoka Kenya.Korir mwendakasi wa pili katika hisoria ya mbio za marathon duniani alijitoa mashindanoni kati kati ya Tokyo marathon baada ya kuumia.