1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Afrika yatafakari kuwa na mahakama yake ya uhalifu wa kivita

14 Julai 2012

Umoja wa Afrika unatafakari suala la kuanzisha mahakama ya bara hilo ya uhalifu wa kivita kuendesha kesi za ukiuaji wa haki za binaadamu katika ardhi ya bara hilo badala ya kuzipeleka barani Ulaya.

https://p.dw.com/p/15Xq4
Mwendesha Mashtaka Mkuu wa ICC Fatou Bensouda
Mwendesha Mashtaka Mkuu wa ICC Fatou BensoudaPicha: AP

Jaji wa mahakama ya Kiafrika ilioko hivi sasa amesema hapo jana mjini Addis Ababa Ethiopia makao makuu ya Umoja wa Afrika kwamba mahakama ya Kiafrika yenye kwashtaki Waafrika itakuwa katika nafasi nzuri zaidi ya kutambuwa tamaduni, mazingira ya kijamii na vitendo vya uhalifu wenyewe.

Mahakama hiyo ambayo haina mamlaka ya kuwafungukia mashtaka wahalifu wa kivita imezitaka nchi wanachama 54 wa Umoja wa Afrika kabla ya kufanyika kwa mkutano wake wa kilele wa mwaka mara mbili unaoanza Jumapili kuyapa nguvu mamlaka yake ili iweze kuwashtaki wahalifu hao wa kivita.

Hata hivyo Rais wa Mahakama hiyo ya Afrika ya Haki za Binaadamu Jaji Garard Niyungeko amesema hata kama Umoja wa Afrika utaidhinisha mapendekezo ya kuipa mahakama hiyo mamlaka zaidi ya kuweza kuwashtaki wahalifu wa kivita itachukuwa miaka mingi kabla ya nchi wanachama kuuridhia uamuzi huo na kuiruhusu mahakama hiyo kufanya kazi.

Amesema hiyo itakuwa agenda katika mkutano wa kilele wa viogozi wa Afrika mjini Addis Ababa, lakini kuweza kujuwa iwapo agenda hiyo itapitishwa au la ni suala jengine.

Rais wa zamani wa Cote d' Ivoire Laurent Gbagbo anashtakiwa na ICC kwa uhalifu dhidi ya ubinaadamu
Rais wa zamani wa Cote d' Ivoire Laurent Gbagbo anashtakiwa na ICC kwa uhalifu dhidi ya ubinaadamuPicha: picture-alliance/dpa

Itafanya kazi vipi?

Haijulikani vipi mahakama hiyo inaweza kufanya kazi kwa kuhusiana na Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu wa Kivita ICC ilioko mjini The Hague Uholanzi, lakini Niyungeko amesema tasisi hizo mbili inabidi ziandae mipango ya kuamuwa ni wapi wanapostahiki kufunguliwa mashtaka wahalifu wa kivita.

Amesema inabidi kwa mahakama zote mbili kulijadili hilo na kuja mpangilio maalumu ili kuepuka kupandiana kwa hukumu.

Mahakama hiyo ambayo hivi sasa kazi zake ni kuilinda katiba ya Umoja wa Afrika kuhusu Haki za Watu na Binaadamu , ilianzishwa hapo mwaka 2004 na makao yake makuu yako mjini Arusha Tanzania. Waraka wake wa itifaki umesainiwa na nchi 26 za Afrika.

Mwendesha Mashtaka Mkuu wa zamani wa ICC Luis Moreno-Ocampo alikuwa akishutumiwa na Afrika kwa kuliandama bara hilo
Mwendesha Mashtaka Mkuu wa zamani wa ICC Luis Moreno-Ocampo alikuwa akishutumiwa na Afrika kwa kuliandama bara hiloPicha: AP

Umuhimu wa mahakama hiyo

Sophia Affuko makamo wa rais wa mahakama hiyo amesema haja ya kuanzishwa kwa mahakama hiyo ya uhalfu wa kivita ya Afrika inatokana na shutuma kwamba mahakama ya ICC imekuwa tu ikifunguwa mashtaka kwa kesi za Afrika.

Affuko amesema dhana iliyoko ni kwamba inawawinda Waafrika kwamba wamewachunguza na kuwafungulia mashtaka Waafrika tu.

Amesema sifa ya kuaminika kwa ICC pia imepata pigo kwa sababu ya kutegemea ushahidi usio wa kuaminika katika kesi zake na kwamba hata uchunguzi wake umekuwa wa kubabaisha haufanywi kitaalamu.

Mwaka huu Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu wa Kivita ICC imemteuwa Fatou Bensouda kutoka Gambia kuwa Mwendesha Mashtaka Mkuu wa mahakama hiyo kuchukuwa nafasi ya Louis Moreno Ocampo kutoka Argentina.

Mwandishi : Mohamed Dahman/AFP

Mhariri: Stumai George