Abu Hamza apelekwa Marekani
6 Oktoba 2012Abu Hamza mzaliwa wa Misri anatuhumiwa na Marekani kwa kuunga mkono kundi la kigaidi la al-Qaeda, kusaidia utekaji nyara nchini Yemen na kupanga kufungua kambi ya mafunzo kwa ajili ya wanamgambo nchini Marekani. Mhubiri huyo mwenye umri wa miaka 54, alifungwa nchini Uingereza kwa kuwachochea wafuasi wake kuwauwa wale aliowaeleza kuwa makafiri, pia alifikia kiwango cha kuvuma kwa ubaya baada ya kusifu shambulio la kigaidi la Septemba 11 lililofanywa dhidi ya Marekani, na alikuwa akiongoza msikiti kaskazini mwa mji wa London ambao Uingereza inasema ni kitovu cha Uislamu wa imani kali.
Ametokea jela
Alichukuliwa kutoka jela yenye ulinzi mkali katikati ya mji wa London katika mlolongo wa magari yaliyokuwa yakilindwa na idadi kubwa ya polisi na kupelekwa katika kituo cha jeshi la anga cha Marekani, ambako alikabidhiwa kwa maafisa wa Marekani na kuwekwa katika ndege kuelekea nchini Marekani.
Hapo mapema , majaji wawili wa mahakama kuu mjini London wametupilia mbali ombi ya kuchelewesha kusikilizwa kwa kesi dhidi yake ili kuweza kumruhusu mhubiri huyo, ambaye hakuhudhuria kikao hicho cha mahakama, ili kufanyiwa uchunguzi wa ubongo, ambapo mawakili wake wamesema utathibitisha kuwa hali yake si nzuri kuweza kupelekwa nchini Marekani.
Badala yake majaji wamesema , "Akifikishwa haraka mahakamani , itakuwa bora zaidi". "Haikubaliki kuwa kesi ya kupelekwa nchini Marekani ichukue muda mfupi , na kupimwa kwa muda wa miezi kadha na sio miaka", wameongeza.
Uingereza imeapa kumrejesha nchini Marekani haraka iwezekanavyo baada ya kutupiliwa mbali kwa rufaa yake. Saa chache baadaye, alikuwa amewekwa katika ndege na yuko njiani kuelekea Marekani.
Wamo na wengine wanne
Watuhumiwa wengine wanne wa ugaidi pia wameshindwa katika rufaa zao dhidi ya kupelekwa nchini Marekani na waliingizwa katika ndege mbili za kiraia za Marekani ambazo zilitolewa na maafisa wa Marekani kuwapeleka watuhumiwa hao nchini humo.
Wameondoka, amesema msemaji wa polisi ya London, ambayo inashughulikia kesi za watu wanaotakiwa katika nchi nyingine .
Kesi zote tano zilipelekwa katika mahakama kuu baada ya mahakama ya haki za binadamu ya umoja wa Ulaya kukataa kuizuwia Uingereza kuwapeleka watu hao nchini Marekani. Akiwa anayehubiri dhidi ya mataifa ya magharibi , Abu Hamza anasemekana kuwa amehamasisha baadhi ya wanamgambo wakubwa duniani ikiwa ni pamoja na Zakaria Moussaoui, mmoja wa watuhumiwa katika kula njama katika shambulio la Septemba 11.
Alikuwa mhandisi mwanafunzi
Amezaliwa akiwa na jina la Mustafa Kamel Mustafa, alihamia nchini Uingereza akiwa mhandisi mwanafunzi katika miaka ya 1970, alioa mwanamke raia wa Uingereza na aliwahi kufanyakazi kama mlinzi wa mlangoni ,"baunsa", katika ukumbi wa disco mjini London.
Abu Hamza ambaye anafahamika sana kwa kuvaa kitu kama ndoana mkononi kutokana na kukatika mkono wake wa kulia, anasema kuwa amepoteza mikono yake yote miwili na jicho wakati akiishi nchini Afghanistan katika miaka ya 1980 akifanyakazi za kiutu. Maafisa wanasema alikuwa akipigana katika kundi la Mujahideen dhidi ya iliyokuwa Urusi ya zamani.
Marekani ilikuwa ikiwahitaji Abu Hamza pamoja na Khalid al-Fawwaz, Adel Abdul Bary, Babar Ahmad na Syed Talha Ahsan ili wafikishwe mahakamani katika mahakama za Marekani kwa madai ya ugaidi.
Mwandishi : Sekione Kitojo / rtre
Mhariri: Iddi Ismail Ssessanga