Zelensky akutana na viongozi wa Marekani, EU mjini Rome
18 Mei 2025
Hiyo ni sehemu ya juhudi zilizoimarishwa za kidiplomasia kabla ya mazungumzo ya simu kesho Jumatatu kati ya Rais wa Marekani Donald Trump na Rais wa Urusi kuhusu kumaliza vita nchini Ukraine.
Zelensky alizungumza na Makamu wa Rais wa Marekani JD Vance na Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Marco Rubio katika makazi ya balozi wa Marekani. Kansela wa Ujerumani Friedriech Merz alisema alizungumza na Zelensky na Rubio pembezoni mwa misa ya kusimikwa rasmi kwa Papa Leo XIV iliyofanyika leo mjini Vatican.
Merz pia amesema amekubaliana na viongozi wa Ufaransa na Uingereza kuwa watazungumza tena na Rais wa Marekani katika maandalizi ya mazungumzo hayo ya simu. Merz amewaambia waandishi habari mjini Rome kuwa viongozi wa Ulaya na Marekani wamedhamiria kushirikiana kuhakikisha vita vinamalizika Ukraine.
Trump alisema anapanga kuzungumza na Putin na kisha Zelensky na viongozi wa nchi mbalimbali za Jumuiya ya NATO, kuhusu kumaliza vita hivyo.