1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Zaidi ya watu 700 wauwawa katika mkanyagano wa hija

Admin.WagnerD24 Septemba 2015

Takriban watu 717 wameuwawa na wengine zaidi ya mia nne wamejeruhiwa katika mkanyagano uliotokea Alhamisi (24.09.2014) wakati Waislamu wakiendelea kutekeleza ibada ya hija nchini Saudi Arabia,

https://p.dw.com/p/1GcSn
Wahanga wa mkanyagano wa hija katika mji wa Mina Saudi Arabia. (24.09.2015)
Wahanga wa mkanyagano wa hija katika mji wa Mina Saudi Arabia. (24.09.2015)Picha: picture-alliance/AP Photo

Mkanyagano huo umetokea katika mji wa Mina bonde kubwa lilioko kama kilomita tano kutoka mji mtakatifu wa Mecca.Mina ulikuwa na mahema zaidi ya 160,000 ambayo yalitumika kwa ajili ya mahujaji waliolala hapo wakati wa usiku.

Kurugenzi ya ulinzi wa kiraia nchini Saudi Arabia imesema takriban watu wengine zaidi ya 800 wamejeruhiwa katika mkanyagano huo.Idadi ya vifo imekuwa kizidi kuongezeka.

Picha zilizotolewa kwenye mtandao wa twitter na kurugenzi hiyo zimeonyesha wafanyakazi wa uokozi wakiwa na vizibao vya rangi ya machungwa na njano wakiwasaidia watu waliojeruhiwa kwa kuwabeba kwenye machela na kuwaingiza kwenye magari ya kubebea wagonjwa karibu na baadhi ya mahema hayo yalioko Mina.

Takriban watu milioni mbili wanashiriki katika ibada ya hija mwaka huu ambayo imeanza hapo Jumanne.

Maafa ni makubwa

Mkanganyagano huo umesasababisha maafa makubwa katika hija kuwahi kushuhudiwa tokea mwaka 2006 ambapo zaidi ya mahujaji 360 waliuwawa katika mkanyagano kwenye eneo hilo hilo.

Wafanyakazi wa uokozi katika juhudi za kuwaokowa mahujaji wa makanyagano Mina Saudi Arabia. (24.09.2015)
Wafanyakazi wa uokozi katika juhudi za kuwaokowa mahujaji wa makanyagano Mina Saudi Arabia. (24.09.2015)Picha: picture-alliance/AP Photo/Saudi Civil Defense agency

Mina ni mahala ambapo mahujaji humipga mawe shetani kwa ishara kwenye nguzo tatu.Waislamu wanatekeleza utaratibu huu wa kumpiga mawe shetani kwa kufuata mfano wa Mtume Ibarahim ambaye inasemekana alimpiga mawe shetani katika maeneo matatu wakati alipojaribu kumshawishi asitimize amri ya Mwenyeenzi Mungu ya kumtowa muhanga mwanawe wa kiume Ismail.

Mkanyagano huo uliotokea leo hii unakuja katika kipindi kisihozidi wiki mbili baaada winchi kubwa ya ujenzi kuanguka kwenye msikiti mkuu wa Mecaa kitovu cha hija ambapo watu 111 waliuwawa na wengine zaidi ya 390 kujeruhiwa.

Hija za huko nyuma zilikuwa zikikabiliwa na mikanyagano na moto iliouwa mamia ya mahujaji lakini katika kipindi cha miaka tisa kwa kiasi kikubwa hija hizo zimekuwa zikifanyika bila ya ajali kubwa kutokana na hatua zilizochukuliwa kuboresha usalama wa mahujaji.

Hija nguzo ya tano ya Uislamu

Hija ni mojawapo ya nguzo tano za Uislamu na kila Muislamu mwenye uwezo anatakiwa kutekeleza ibada hiyo angalau mara moja katika uhai wake.Kwa Waislamu wengi hicho ni kilele cha imani yao ya kidini.

Mahujaji wakia karibu na Mlima Arafa.(23.09.2014)
Mahujaji wakia karibu na Mlima Arafa.(23.09.2014)Picha: Getty Images/AFP/M. Al-Shaikh

Hija hiyo ilianza Jumanne wakati mahujaji walipoingia "ihram" hali ya kujitakasa ambapo wanatakiwa wasigombane, wasijipake manukato au kukata kucha na nywele zao.

Wakati wa Ihram wanaume huvaa shuka mbili nyeupe moja kiunoni na moja begani ambapo wanawake wanatakiwa wavae mavazi meupe yasiowabana na nyuso tu na viganya vyao vya mkono tu ndio vinavyotakiwa kuwa wazi.Mavazi hayo yaashiria umoja wa mahujaji bila ya kujali utaifa wao au madaraja yao wawe matajiri au maskini.

Takriban mahujaji wa kigeni milioni 1.4 wanaungana na wenzao mamia kwa maelfu Wasaudi na wakaazi wengine wa nchi hiyo ya kifalme kwa ajili ya ibada ya hija ya mwaka huu.

Mwandishi : Mohamed Dahman/AP/AFP

Mhariri : Iddi Ssessanga