1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wenyeji Urusi waicharaza Saudi Arabia

Bruce Amani
15 Juni 2018

Urusi ilianza michuano yake ya Kombe la Dunia katika njia ya kipekee, kwa kuirarua Saudi Arabia mabao matano kwa sifuri mbele ya umati wa nyumbani mjini Moscow

https://p.dw.com/p/2zb7V
Russland, WM 2018: Russland-Saudi Arabien
Picha: Reuters/C. Recine

Putin aliuambia umati wa karibu watu 80,000 katika uwanja wa Luzhniki kabla ya mchuano wa ufunguzi kuwa na namnukuu "mapenzi ya kandanda huunganisha ulimwengu mzima na kuufanya kuwa timu moja, bila kujali lugha za watu au nadharia”.

Kisha baada ya hapo shughuli ikaanza uwanjani. Huku wakitiwa motisha na mashabiki wa nyumbani, mchezaji aliyeingia kama nguvu mpya Denis Cheryshev alifunga mabao mawili na kuisaidia Urusi ambayo ndiye mwenyeji wa dimba kuongoza Kundi A.

Ulikuwa ushindi wa kwanza wa Kombe la Dunia kwa Uusi tangu mwaka wa 2002 na uliomaliza mfululizo wa mechi saba za bila kupata ushindi.

Russland, WM 2018 Eröffnungsfeier
Putin na wageni wake katika uwanja wa LuzhnikiPicha: picture-alliance/TASS/A. Druzhinin

Awali Yuri Gazinky aliiweka Urusi kifua mbele kwa kufunga bao la kichwa katika dakika ya 12 baada ya Wasaudi kushindwa kuondoa kona. Cheryshev la pili katika dakika ya 43 kabla ya Artyom Dzyuba kufunga bao la tatu kwa kichwa mara tu baada ya kuingia uwanjani kama nguvu mpya katika dakika ya 71. Golon alifunga la tano kupitia free kick. Saudi Arabia ambao walishinda mechi yao ya mwisho katika Kombe la Dunia mwaka wa 1994, hawakuwa na mkwaju wowote uliolenga kwenye goli. Kwa mara ya kwanza katika Kombe la Dunia, mfumo wa refarii msaidizi wa video ulitumika isipokuwa haukiwa na kazi yoyote kubwa katika mechi ya ufunguzi jana.

Siku ya pili ya uhondo wa Kombe la Dunia itahusisha mojawapo ya mechi zinazisubiriwa kwa hamu kabisa katika duru ya ufunguzi. Uhispania dhidi ya Ureno katika Kundi B. Uhispania inaingia katika mechi hii baada ya maandalizi yao kutumbukizwa katika mparaganyiko. Kocha wao Julen Lopetegui alitimuliwa na shirikisho la kandanda la Uhispania na nafasi yake kuchukuliwa na Fernando Hiero ambaye amekuwa akihudumu kama mkurugenzi wa spoti wa timu hiyo. Lopetegui alifutwa kwa sababu alikubali kazi ya kuifundisha Real Madrid.

Russland, WM 2018 Eröffnungsfeier Robbie Williams
Burudani la ufunguzi wa Kombe la DuniaPicha: Getty Images/C. Rose

Mechi nyingine mbili za leo zitakuwa kati ya Misri na Uruguay katika Kundi A na Morocco dhidi ya Iran katika Kundi B. Misri inashiriki katika Kombe la Dunia kwa mara ya kwanza baada ya miaka 28 na mafanikio yake yatategemea afya ya nyota wa Liverpool Mohamed Salah, aliyejeruhiwa katika fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya lakini anatarajiwa kucheza.

Kocha wa Misri Hector Cuper amesema Salah amepona na kuwa kurejea kwake kunaipiga jeki Misri na pia dimba hilo nchini Urusi kwa sababu kuna maana mmoja wa wachezaji ambao ni moto wa kuotea mbali ulimwenguni kwa sasa atakuwa uwanjani.

Kocha wa Morocco Herve Renard ana matumaini kuwa amefanya kazi yake vizuri ya kujiandaa dhidi ya Iran na kuwa ukosefu wake wa uzoefu katika Kombe la Dunia hautamuathiri wakati timu hizo mbili zitakapoanza kukwaruzana.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP/DPA
Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman