1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

WASHINGTON : Vitu vya kuchezea vyaondolewa sokoni

15 Agosti 2007
https://p.dw.com/p/CBZ6

Kampuni kubwa kabisa ya kutengeneza vitu vya kuchezea ya Marekani Mattel inaviondowa kwenye soko duniani kote vitu vya kuchezea watoto milioni 18 vilivyotengnezwa nchini China nusu yake vikiwa nchini Marekani pekee.

Vitu hivyo inaelezwa kwamba vina smaku ambayo inaweza kumezwa na watoto au vinaweza kuwa vimepakwa madini ya risasi. Mwenyekiti wa Kamisheni ya Walaji ya Usalama wa Bidhaa nchini Marekani Nancy Nord ametangaza hapo jana mjini Washington kwamba hatua hiyo iliochukuliwa ni ya hiari.

Amesema katika kukabiliana na tatizo hilo kampuni imezuwiya mauzo na kuagiza bidhaa zote ziondolewe kwenye maduka ya reja reja pamoja na kufanya mabadiliko ya uzalishaji wa bidhaa katika kulishughulikia suala hili.

Hii ni mara ya pili kwa kampuni hiyo ya Mattel kuziondowa bidhaa kwenye masoko katika kipindi kisichozidi wiki mbili na ni dosari nyengine kwa bidhaa za China ambayo hivi karibuni imekabiliwa na hatua kadhaa za kuondolewa kwa bidhaa zake kwenye masoko kuanzia na matairi ya magari yanye kasoro hadi dawa ya meno iliovunda.