1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wapiganaji 265 wa Ukraine wajisalimisha kwa Urusi

17 Mei 2022

Urusi imesema mamila ya wapiagani wa Ukraine 265 waliokuwa wamejificha kwenye kiwanda cha chuma cha Azovstal kwenye mji wa Mariupol kwa wiki kadhaa sasa, wamejisalimisha chini ya makubaliano yaliofikiwa na Kyiv.

https://p.dw.com/p/4BQfd
BG Ukraine - Freiwillige Helfer und mobile Krankenhäuser
Picha: JORGE SILVA/REUTERS

Wizara ya ulinzi ya Urusi ilisema katika taarifa yake kwamba katika kipindi cha saa 24 zilizopita wapiganaji 265 wa Ukraine waliweka silaha zao chini na kujisalimisha, kati ya hao 51 walikuwa wamejeruhiwa vibaya, hivyo kupelekwa katika maeneo ambayo yanadhibitiwa na washirika wa Moscow kwa ajili ya kupatiwa matibabu kwa haraka.

Urusi ilichapisha picha zikiwaonesha askari wa Ukraine wakiwa wamebebwa kwenye machela, wakipandishwa kwenye mabasi huku wengine wakisakwa kwenye maeneo ya maficho yao katika kiwanda cha chuma cha Azovstal kilichoshuhudia mashambulio makali ya vikosi vya Urusi kwa juma kadhaa sasa.

Mapema leo Ukraine ilithibitisha taarifa hizo kupitia wizara yake ya ulinzi na kuonesha tumaini lake la  kutimiza kile walichokubaliana kabla ya kufikia uamuzi wa kuwahamisha wapiganaji hao wa kubadilishana wafungwa ili kuwarejesha nyumbani wapiganaji hao wa Ukraine.

Soma zaidi:Urusi,Ukraine waafikiana kuwaondoa wanajeshi Azovstal

Hata hivyo Spika wa bunge la Urusi Yacheslav Volodin amesema kwenye mtandao wa Telegrama, wahalifu wa ki- Nazi hawapaswi kuwa chini ya makubaluiano ya kubadilishana wafungwa na kuongeza kwamba wanafanya linalowezekana ili kuwafikisha mbele ya sheria.

Urusi yaongeza mashambulizi katika kambi ya jeshi ukrainer

Katika hatua nyingine msemaji wa huduma za dharura za mkoa wa Chernigiv, Oleksandr Ivchenko amesema, mashambulizi ya Urusi leo Jumanne yamekilenga kijiji kimoja kilichopo kaskazini mwa Ukraine Desna ambacho ni kituo cha kijeshi cha Ukraine na kusababisha vifo vya watu wanane na wengine 12 kujeruhiwa.

Ukraine russischer Militäreinsatz in Ostukraine |   Mariupol
Sehemu ya shambulio la vikosi vya Urusi UkrainePicha: Sergei Grits/AP Photo/picture alliance

Kando na Urusi kuendeleza mashambulizi yake, Kyiv imesema mazungumzo ya amani ya kusitisha mapigano na Urusi nchini Ukraine yamesitishwa na kuilaumu Moscow kwa kushindwa kufikia lengo hilo.

Mykhaylo Podolyak Msaidizi wa Rais ambae pia ni mpatanishi mkuu katika mazungumzo hayo na ujumbe wa Urusi amesema, Moscow imepofushwa na mtazamo wake hasi.

Soma zaidi:Urusi yaushambulia mji wa Odesa

Naibu waziri wa mambo ya nje wa Urusi Andrei Rudenko amenukuliwa na shirika la habari la Intarfax akisema kwamba mazungumzo hayakufanyika kwa njia yoyote kati ya pande hizo mbili zilizoingia kwenye mzozo mbaya zaidi kuwahi kushuhudiwa ulaya tangu vita vya pili vya dunia.

ICC yatuma timu ya wataalamu kufanya uchunguzi.

Mahakama ya kimataifa ya Uhalifu leo jumanne imetuma nchini Ukraine timu ya wataalamu 42  ili kuchunguza madai ya uhalifu wa kivita tangu Urusi ilipoivamia Ukraine mwishoni mwa mwezi Februari.

Kikosi hicho kimejumuisha wachunguzi, wataalam wa kutafuta vyanzo vya uhalifu ambao watafanya kazi kwa ukaribu na mamalaka za Ukraine.

Ukraine Butscha | Karim Khan, Internationaler Strafgerichtshof
Mwendesha mashtaka mkuu wa ICC Karim Khan akiwa na mwendesha mashatka mkuu wa Ukraine Iryna VenediktovaPicha: Volodymyr Petrov/REUTERS

Soma zaidi:Ukraine inaandaa kesi kadhaa za uhalifu wa kivita

Mwendesha mashtaka mkuu wa ICC Karim Khan alisema kwenye taarifa yake kwamba, kikosi hicho ni kikubwa zaidi kuwahi kutumwa na ofisi yake kwa ajili ya kuendesha uchunguzi

"Timu itaendesha uchunguzi uchunguzi kwa ajili ya mahakama na kutoa msaada kwa mamalaka ya kitaifa ya Ukraine" Aliongeza sehemu ya taarifa yake.

Aliongeza kwamba wachunguzi hao wa ICC watakuwa na jukumu la kutafuta visa na kukusanya ushahidi kutoka kwa mashahidi kuhusina na mashambulizi ya kijeshi.

Mwendesha mashtaka huyo wa ICC alitangaza uchunguzi kuhusu uhalifu wa kivita na uhalifu dhidi ya binadamu siku nne tu baada ya uvamizi wa Urusi Februari 24.