1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wamarekani wapiga kura Leo.

Ponda, Eric Kalume3 Novemba 2008

► Baada ya muda wa miezi 20 ya kampeini, mijadala, matangazo kwenye vyombo mbali mbali vya habari, hatimaye raia wa Marekani wanapiga kura leo kumchagua Barrak Obama au John McCain kuwa Rais mwakani.

https://p.dw.com/p/Fmne
Barrak Obama wa chama cha Demokrat na John McCain wa Republican, kujulikana mbivu na mbichi leo.Picha: AP / DW Montage



Kote nchini humo shughuli inatarajiwa kuanza kupamba moto huku maafisa wa serikali wakijiandaa kwa milolongo mirefu ya wapiga kura katika vituo mbali mbali vya kupigia kura.


Uchaguzi wa leo unatajwa kuwa wa kihistoria kwani iwapo seneta John McCain mwenye umri wa miaka 71 atashinda atakuwana rais wa kwanza mwenye umri mkubwa kuingia uongozini kwa kipindi cha kwanza, huku Senta Barrak Obama mwenye umri wa miaka 47 atakuwa rais wa kwanza mwenye asili ya Kiafrica kuliongoza taifa hilo.


Wadadisi wanakadiria kuwa kati ya asilimia 80 na 90 ya wapiga kura watajitokeza kupiga kura ikilinganishwa na asilimia 60 wakati wa uchaguzi mkuu uliopita mwaka wa 2004, ambapo hii ndio idadi kubwa zaidi ya wapiga kura kuwahi kushuhudiwa nchini Marekani tangu mwaka wa 1968.


Iwapo ni Seneta John McCain au Barak Obama atakayechaguliwa kuliongoza taifa hilo lenye uwezo mkubwa ulimwenguni, hatakuwa na kibarua rahisi hasa ikizingatiwa kwamba, uchaguzi huu unafanyika wakati ambapo Marekani imekumbwa na mzozo wa kifedha uliotingisha masoko ya fedha katika mataifa mengi ulimwenguni.


Mbali na hayo, rais atakayechaguliwa atakuwa na jukumu kubwa la kurejesha hadhi ya taifa hilo, iliyochafuka wakati wa kipindi cha miaka 8 ya utawala wa rais wa sasa George W.Bush.

Tayari mamilioni ya wapiga kura wamepiga kura zao katika muda wa wiki chache zilizopita hasa katika majimbo 31, yakiwemo majimbo yanayong´ang´aniwa sana kwenye uchaguzi huu, ya Florida, North Carolina, Colorado na Naveda.


Kwa wakati huu kura ya maoni inaonyesha Barrak Obama akiongoza kwa jumla ya asilimia 50.7 dhidi ya John McCain aliye na asilimia 44.3


Kampeini za wagombea hao wawili zimezingatia zaidi masuala ya uchumi, huku mgombea wa chama cha demokrat Barrak Obama akiulaumu utawala wa miaka minane wa chama cha Republican kwa kuzorotesha uchumi.

Kwa upande wake, Senta John McCain amekuwa akimshtumu Barrak Obama kwa kutumia kiasi kikubwa cha pesa kwa ajili ya Kapeini,baada ya mbinu za upande wa McCain kumtaja Obama kuwa mtu anayeshirikiana na magaidi,kuambulia patupu.


Cha kushangaza ni kwamba rais George Bush na makamu wake wa rais Dick Cheney hawakujitokeza kumsaidia McCain katika kapeini zake, isipokuwa tu mwishoni mwa wiki ambapo Dick Cheney alionekana hadharani kumfanyia kampeini John McCain.


Katika kampeini zake Barrak Obama amesisitiza kuleta mabadiliko katika sera na maongozi ya kigeni kuhusiana na vita nchini Iran na Afghanistan, Iran na hata Korea Kusini.


Kutokana na hali ilivyo kwa sasa, hapana shaka kiongozi atakayechaguliwa atakuwa na jukumu kubwa la kurejesha hadhi ya taifa hilo kama taifa lenye uwezo mkubwa ulimwenguni.