1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wakili wa Rais wa zamani wa Iraq, ajitokeza kumtetea mwandishi aliyemtukana Rais Bush.

Halima Nyanza15 Desemba 2008

Aliyekuwa Wakili wa Rais wa zamani wa nchi hiyo, Saddam Hussein amejitokeza kuweza kumtetea, mwandishi aliyekamatwa baada ya kumrushia viatu Rais Bush mjini Baghdad.

https://p.dw.com/p/GGhp
Rais George W Bush wa Marekani akikwepa viatu alivyokuwa akirushiwa na Mwandishi wa Habari wa Iraq, wakati wa mkutano wake na wanahabari mjini Baghdad.Picha: AP

Wakili huyo mwenye makao yake mjini Amman, Jordan, Khalil Al Dulaimi amesema mpaka sasa Wairaq 200 na mawakili wengine, wakiwemo Wamarekani wameelezea nia yao ya kutaka kumtetea mwandishi huyo wa habari wa Iraq, ambaye alimtupia kiatu Rais Bush wakati alipofanya ziara ya mwisho na ya kuaga mjini Baghdad.

Amesema alifikia uamuzi wa kumtetea mwandishi huyo jana usiku baada ya kutokea kwa tukio hilo pamoja na kutoa wito wa kuachiwa mara moja.

Wakili Dulaimi alikuwa akiongoza timu ya mawakili wa Saddam Hussein mpaka pale hukumu yake ilipotekelezwa Desemba mwaka 2006.

Mwandishi huyo kutoka katika kituo kimoja binafsi cha Televisheni nchini humo cha Al Baghdadiya, Muntazer Al Zaid aliinuka alipokaa wakati Rais Bush akizungumza na wanahabari, kwa pamoja na Waziri Mkuu wa nchi hiyo Nuri Al Maliki jana Jumapili, na kupaza sauti kumtukana Rais Bush na baadaye kumrushia viatu.

Lakini hata hivyo Rais Bush aliweza kukepwa viatu hivyo vilivyorushwa dhidi yake, na kwamba walinzi walimkamatwa mwandishi huyo.

Baadhi ya Wairaq, wanaounga mkono kitendo cha mwandishi huyo wa habari kumtukana Rais Bush, wanasema hiyo imetokana na yale aliyokuwa akiyasema Rais huyo wa Marekani kuhusiana na kuijenga upya Iraq na kuimarishwa kwa demokrasia, kwamba siyo kweli.

Kitendo cha mwandishi huyo, kumrushia kiatu Rais Bush, kimepokelewa kwa hisia, katika eneo la Mashariki ya kati, ambapo wengi wanamuona kama shujaa na kutaka aachiiliwe huru, ambapo wengine wanasema ni jinsi inavyoonesha Wairaq na Warabu kwa ujumla wanavyomchukia Rais Bush, kutokana na kudaiwa kusababisha vifo vya maelfu ya Wairaq baada ya majeshi yake kuivamia nchi hiyo.

Baada ya kuaga nchini Iraq, leo Rais Bush alikwenda kuaga pia Afghanistan na kuonya kwamba bado kunasafari ndefu kuweza kuleta utulivu nchini humo, ambako wanajeshi wa kigeni wapatao elfu 70 wamekuwa wakipambana na wapiganaji.

Hata hivyo amesema hali kwa sasa ni bora kuliko ilivyokuwa mwaka 2001, mwaka ambao utawala wa Taliban uliondolewa.