1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wahariri washauri mwafaka baina ya Merkel na Hollande

Abdu Said Mtullya9 Mei 2012

Wahariri wanazungumzia juu ya mafanikio katika harakati za kupambana na magaidi wa Al-Qaeda na mjadala juu ya kubana matumizi na kuleta ustawi

https://p.dw.com/p/14sBY
Kansela wa Ujerumani Angela Merkel
Kansela wa Ujerumani Angela MerkelPicha: dapd

.Gazeti la"Reutlinger General-Anzeiger"linazungumzia juu ya harakati za kupambana na magaidi wa Al-Qaeda. Hata hivyo linasema pana pande mbili za ukweli. Kwanza inafaa kutilia maanani ufanisi uliofikiwa katika juhudi za kupambana na magaidi hao .Ni ufanisi ulioje,kuona jinsi idara za usalama zinavyofanikiwa kuzigundua njama za kufanya mshambulio ambayo yangeliweza kuleta maafaa makubwa.

Lakini gazeti la "Reutlinger General-Anzeiger "linasema katika upande mwingine ni muhimu kutahadharisha juu ya wale wanaoweka chuki mbele,badala ya stahamala na utayarifu wa kufanya mazungumzo. Itakuwa ni kujidanganya kufikiri kwamba ugaidi umetoeka duniani baada ya Osama Bin Laden kuuliwa.

Mhariri wa gazeti la "Saarbrücker" pia anasema,kuwa mafanikio yamefikiwa katika harakati za kupambana na magaidi duniani, lakini linatahadharisha kwamba hakuna sababu ya kulegeza kamba. Ukweli ni kwamba wakati uongozi wa makao makuu ya magaidi nchini Afghanistan na Pakistan umepondeka , kiasi cha kutokuwa na nguvu ya kutenda makubwa,tawi lao linastawi katika Yemen,yaani nchi isiyokuwa imara kisiasa ,kama iliyvokuwa Afghanistan, kabla ya majeshi ya Nato kuivamia. Hakuna anaeweza kuukwepa ukweli huo, kwani kufanya hivyo kunaweza kuwa kosa la hatari kubwa.

Mhariri wa "Saarbrücker" anakumbusha kwamba Yemen ndiyo chimbuko la njama za hivi karibuni, za kufanya mashambulio katika ndege za abiria. Kwa kuwa sasa, hakuna njia nyingine ya ufanisi ya kupambana na magaidi nchini Yemen, Rais Obama atafanya jambo la manufaa kuimarisha mashambulio ya ndege zisizokuwa na rubani nchini Yemen.

Gazeti la "Mittelbayerische" linatoa maoni juu ya mkingamo uliopo baina ya watetezi wa sera za kubana matumizi na wale wanaotaka fedha zaidi ziekezwe ili kuleta ustawi. Gazeti hilo linaeleza kwamba bara la Ulaya limesimama njia panda. Serikali zinapaswa kuleta uwizani baina ya mipango ya kubana matumizi na kuleta ustawi. Kwa sababu mshuko wa uchumi na kiwango kikubwa cha ukosefu wa ajira kutaharakisha mwendo wa kuangukia katika maafa.

Katika muktadha huo, mkutano ujao baina ya Kansela wa Ujerumani Angela Merkel na Rais mteule wa Ufaransa Francois Hollande ni muhimu sana.Hollande anatetea siasa ya kuleta ustawi wakati Merkel anataka nidhamu ya bajeti.Viongozi hao watapaswa kukaribiana kwa namna fulani katika misimamo yao.

Na mhariri wa gazeti la "Rhein Zeitung" anasisitiza katika maoni yake kwamba hakuna mkingamo baina ya sera za kubana matumizi na kuleta ustawi.Hiyo ni hoja moja yenye pande mbili. Lakini nchi zenye madeni haziwezi kuepuka sera za kubana matumizi kwani ndiyo msingi wa kuimarisha ushindani.

Mwandishi:Mtullya Abdu/Deutsche Zeitungen/

Mhariri: Yusuf Saumu