1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wahariri wasema Breivik ni mnyama

Abdu Said Mtullya17 Aprili 2012

Wahariri wa magazeti karibu wote wanamzungumzia gaidi wa Norway aliyeziangamiza roho za watu 77 nchini humo.Kesi ya mnyama huyo inaendelea leo.

https://p.dw.com/p/14f9Q
Muuaji Anders Behring Breivik mahakamani mjini Oslo
Muuaji Anders Behring Breivik mahakamani mjini OsloPicha: Reuters

Hapo jana alikiri mbele ya mahakama kuwa aliwaua watu hao 77, lakini aliyakana mashtaka ya mauaji. Gazeti la "Mai Post" linasema katika maoni yake kwamba mnyama huyo ameanza kuuonyesha uso wake halisi alipodai kwamba aliwaangamiza watu hao 77 kama hatua ya kujihami. Anayosema yanasababisha mshangao mkubwa, kwani amewaua, wale wale ambao anadai alikusudia kuwalinda dhidi ya uislamu.Mtu hawezi kuwa mwokozi wa dunia ile ile anayoiangamiza.


Mhariri wa gazeti la "Saabrücker" anasema,kwa muda wa wiki kadhaa Breivik atakuwa anayafafanua mawazo yake mbele ya mahakama .Jambo ambalo litakuwa karaha kwa wale waliowapoteza ndugu zao. Lakini anasema huo ndio mfumo wa sheria katika nchi za kidemokrasia. Mhariri huyo anaeleza kwamba waliowapoteza ndugu zao watakuwa katika hali ya mateso moyoni kwa muda wote wa kesi inayomkabili Breivik. Hakika mfumo wa sheria katika nchi ya kidemokrasia mara nyingine ni mtihani mkubwa.Lakini hakuna njia ya kuzuia hatari ya kutokea vitimbi vya kiholela mahakamani.

Gazeti la"Flensburger Tageblatt" linasema kesi inayomkabili muuaji Breivik ni hatua ya lazima katika juhudi za kukabiliana na uhalifu. Gazeti hilo linafafanua kwa kusema kwamba uhalifu uliotokea umetendwa na mtu wa kawaida mwenye mizizi iliyomo katika jamii huru. Jambo hilo linapaswa kuzingatiwa. Na mahakamani ni mahala panapostahili. Kitakachosaidia katika juhudi za kuepusha uhalifu kama huo kutokea tena ni hatua madhubuti .Ni kazi ngumu kwa wote, lakini hatimaye hiyo inaweza kuwa tiba.

Gazeti la "Financial Times Deutschland" linatoa maoni juu ya mgogoro wa madeni unaoikabili Uhispania, kwa kuelezea wasi wasi juu ya kurejea tena kwa mgogoro huo barani Ulaya. Gazeti hilo linauliza jee mgogoro wa Euro unarejea tena barani Ulaya kwa nguvu zote. ? Linasema dalili zinaonyesha kwamba Benki Kuu ya Ulaya haina uwezo wa kutosha wa kuepusha kiherehere. Benki hiyo imetoa mikopo ya Euro Bilioni 100 kwa mabenki kwa riba za chini kwa kipindi cha miaka mitatu.Kila benki ina uamuzi wake.Inaweza kuwekeza katika dhamana za Uhispania na Italia.

Lakini ikiwa mabenki hayo yataondoa vitega uchumi kwa njia ya pupa,kiwango cha riba kitapanda juu haraka. Sasa ni inapasa kwa serikali za Umoja wa Ulaya pamoja na Benki kuu kufanya matayarisho endapo inatokea dharura!

Tafsiri Abdu Mtullya/Deutsche Zeitungen

Mhariri: Yusuf Saumu