1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

WADA yapinga wanamichezo kufungwa jela

17 Novemba 2014

Shirika la kimataifa la kupambana na matumizi ya dawa za kuongeza nguvu mwilini – WADA limesema linapinga hatua ya kuwawekea makosa ya uhalifu wanariadha wanaogundulika kutumia dawa hizo

https://p.dw.com/p/1Dojq
Chicago Marathon 2013 Rita Jeptoo
Picha: picture-alliance/dpa/Tannen Maury

Hiyo ni licha ya kuwepo sheria kali ambayo itaanza kutekelezwa Januari mosi. Katika mkutano wa wanachama wake hapo jana, WADA pia imetangaza kuwa ahadi za kuanzishwa mfuko maalum wa fedha za utafiti wa matumizi ya dawa zilizopigwa marufuku zimefika zaidi ya dola milioni kumi na kutoshana na uwekezani uliofanywa na Kamati ya Kimataifa ya Olimpiki. Mradi huo wa pamoja hivyo basi utakuwa na bajeti ya karibu dola milioni 20.

Rais wa WADA Craig Reedie anasema mwanariadha anastahili kuadhibiwa chini ya sheria za michezo ambazo zimekuwepo kwa miaka mingi, badala ya kuadhibiwa na sheria ya uhalifu.

Symbolbild Doping
Ujerumani inatayarisha sheria kali ya kupambana na dawa za kuongeza nguvu mwiliniPicha: picture-alliance/dpa/U. Anspach

Shirika hilo limesema linajitahidi kuhakikisha kuwa maabara ya Rio de Janeiro inapewa tena kibali cha kutumiwa katika Michezo ya Olimpiki ya mwaka wa 2016. Sheria mpya dhidi ya matumizi ya dawa zilizopigwa marufuku itawaadhibu watakaopatikana na makosa kwa mara ya kwanza kwa kuwapiga marufuku kwa kipindi cha miaka minne badala ya miaka miwili.

Reedie amejitenga na rasimu ya muswaada wa Ujerumani, ambao unataja kifungo cha hadi miaka mitatu kwa wanariadha wa kulipwa watakaopatikana wakitumia dawa zilizopigwa marufuku michezoni. Muswada huo unatarajiwa kupelekwa katika Baraza la Mawaziri ili kuidhinishwa mwezi Aprili.

WADA ilivibatilisha vibali vya maabara ya kuchunguza madawa mjini Rio de Janeiro mwaka jana kwa sababu ilishindwa kutimiza viwango vya shirika hilo.

Rita Jeptoo ni miongoni mwa wanariadha maarufu nchini Kenya waliogundulika kutumia dawa zilizopigwa marufuku. WADA hivi karibuni ilikutuna na maafisa wa Kenya mjini Cape Town ili kuwasaidia kuanzisha Shirika la Kupambana na matumizi ya Dawa zilizopigwa marufuku nchini Kenya huku mashirika ya Norway na China yakitoa mafunzo ya kiufundi na mwongozo.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP/Rueters
Mhariri: Yusuf Saumu