1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wabunge wa Ulaya walalamika

Hamidou, Oumilkher2 Septemba 2008

Wabunge wa Ulaya wanataka Georgia pia ikosolewe

https://p.dw.com/p/FAA2
Mchanganyiko wa bendera ya Umoja wa ulaya na ile ya UrusiPicha: DW-Montage/Bilderbox.de



 Wabunge wa Ulaya wameukosoa Umoja wa ulaya hii leo kwa kile kilichotajwa kua "kuihurumia zaidi Georgia,na kutozungumzia mchango wa Tblisi katika mzozo pamoja na Urusi.Lawama hizo zimefuatia mkutano wa dharura wa kilele wa Umoja wa ulaya ulioitishwa mjini Brussels kuzungumzia mzozo huo.



"Maamuzi yaliyopitishwa katika mkutano huo wa kilele,yalikua pengine yakielemea zaidi upande mmoja" amesema mwenyekiti wa kundi la waliberali katika bunge la Ulaya,Graham Watson wa kutoka Uengereza,anaezusha uwezekano wa kufikiwa makubaliano kati ya wale wanaotaka vikwazo viwekwe dhidi ya Urusi na wengineo wanaopendelea mazungumzo yaendelezwe pamoja na Moscow.


"Nnaamini kuna makubaliano yaliyofikiwa pamoja na Poland na mataifa ya Baltic ili yakubali Urusi isiwekewe vikwazo,kwa sharti Georgia haikosolewi."Amesema hayo Graham Watson wakati wa mkutano pamoja na waandishi habari hii leo mjini Bruxelles.


"Katika taarifa yao ya mwisho,viongozi wa umoja wa ulaya hawajasema chochote kuhusu Georgia" amelalamika kwa upande wake mwenyekiti mwenza wa kundi la wabunge wa walinzi wa mazingira Daniel Cohn-Bandit anaesema tunanukuu: "ingekua vyema kuwalaumu wote wanaofikiri mzozo unaweza kutatuliwa kwa mtutu wa bunduki."


"Inaonyesha ni hakika kwamba sehemu ya msaada wa fedha zinazotolewa na Umoja wa ulaya kwa Georgia,kabla ya mzozo kuripuka,imetumiwa vibaya na kugharimia silaha" amelalamika mwanasiasa huyo wa kutoka chama cha walinzi wa mazingira anaehoji "vyombo vya habari vimefanya uchunguzi kuhusu madai hayo."


Msemaji wa halmashauri kuu ya Umoja wa ulaya amesema kwa upande wake "hana habari zozote kuhusu uchunguzi huo na kusisitiza wakati huo huo misaada ya fedha ya Umoja wa Ulaya haigharimii mahitaji ya kijeshi."


Nae muakilishi wa kundi la wahafidhina katika bunge la Ulaya Joseph Daul wa kutoka Ufaransa amesema ameridhika na uamuzi wa viongozi 27 wa umoja wa ulaya wa kuakhirisha mazungumzo kuhusu ushirikiano wa kimkakati pamoja na Urusi na kujadiliana kinaga ubaga na Urusi.Amesema hata hivyo kuna baadhi miongoni mwa wabunge wa kihafidhina wanaouangalia uamuzi huo kua ni mkali mno na wengine wanaohisi ni dhaifu.


 Muakilishi wa siasa ya nje wa Umoja wa ulaya Javier Solana anasema.


"Nnafikiri tunaelekea ndiko.Njia za mawasiliano pamoja na Urusi tumeziacha wazi.Ni nchi muhimu.Na tunataraji majadiliano ya wiki ijayo pamoja na Moscow yatatufungulia njia ya kuendelea kushirikiana."


Busara ndio iliyoibuka na ushindi" amesema hayo waziri mkuu wa Urusi Vladimir Putin,alipokua akizungumzia matokeo ya mkutano wa kilele  wa viongozi wa Umoja wa ulaya uliofanyika jana mjini Brussels.


"Hatujaona kama kuna pendekezo lolote lililofurutu,kinyume na misimamo mikali iliyojitokeza wakati wa maandalizi ya mkutano huo" amesema hayo waziri mkuu wa Urusi Vladimir Putin akiwa ziarani Tachkent.