Wabunge wa Ujerumani wamewasili Iran
17 Oktoba 2010TEHERAN:
Ujumbe wa wabunge wa Ujerumani umewasili mjini Teheran ili kufanya juhudi za kuwatoa waandishi habari wawili wa Ujerumani waliokamatwa na kutiwa ndani nchini Iran.
Katika muda wa siku tano zijazo wabunge hao wamepangiwa kukutana na wabunge wenzao,viongozi wa serikali, wawakilishi wa asasi zinazotetea haki za binadamu na wasanii.Wajerumani hao wawili walikamatwa wiki iliyopita baada ya kumhoji mtoto wa mwanamke aliehukumiwa adhabu ya kifo kwa kupigwa mawe kwa kosa la kukiuka ndoa.
Idara za serikali za Iran zinadai kwamba waandishi hao walifanya mahojiano na mtoto wa mama huyo bila ya kibali.Walikamatwa katika mji wa Tabriz kaskazini magharibi mwa Iran walipoingia wakiwa na vibali vya kitalii.
Ijumaa iliyopita shirika la habari la serikali ya Iran liliarifu kuwa wajerumani hao walikiri kutenda kosa la jinai.
Shirika hilo lilimnukulu mwendesha mashtaka wa serikali akisema kuwa watu hao waliingia nchini wakiwa na viza za kitalii lakini walijitambulisha kama waandishi wa habari bila ya kutoa ushahidi kabla ya kuwasiliana na familia ya Sakineh Mohammadi-Ashtiani- mwanamke aliehukumiwa adhabu ya kifo kwa kupigwa mawe.