1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Waasi wa M23 warejea Congo

Sekione Kitojo
16 Januari 2017

Waasi wenye silaha nchini Congo wameingia tena nchini humo kutoka katika nchi jirani ya Uganda, na kuzusha hofu kwamba mapigano ya chini kwa chini ambayo yalifikishwa mwisho mwaka 2013 yanaweza kuanza tena.

https://p.dw.com/p/2VsPJ
M23 Rebellen erobern Ostkongos Stadt Goma
Waasi wa kundi la M23Picha: DW/S. Schlindwein

Karibu  wapiganaji  200  wa  kundi  la  M23 , kundi  la  Watutsi  walio jamii  ya  wachache  lililoshindwa  na  jeshi  la  Jamhuri  ya kidemokrasi  ya  Congo  miaka  mitatu  iliyopita , wamewasili  kutoka Uganda  na  kukamata  kijiji  kimoja  kaskazini  mwa   jimbo  la  Kivu ya  kaskazini, msemaji  wa  serikali  ya  Congo Lambert Mende ameliambia  shirika  la  habari  la  Ufaransa  afp.

Mende  amesema  jeshi  la  Congo  linapambana  na  vikosi  viwili vilivyopelekwa  katika  kijiji  cha  Ishasha ambavyo  vilitarajiwa  kuwa nchini  Uganda  chini  ya  uangalizi  wa  maafisa  wa  nchi  hiyo.

M23 Rebellen erobern Goma
Wapiganaji wa kundi la M23Picha: Simone Schlindwein

"Ni  vipi  majirani  zetu  wa  Uganda , ambao  tuna  mipaka  nao wakiwajibika  kabisa, wameweza  kuruhusu   watu  ambao  walikuwa wanaishi  katika  makambi  ya  wakimbizi  kuvuka  mpaka  na  silaha , hadi  katika  ardhi  yetu?"  ameongeza.

Serikali  ya  Congo  imesema  jenerali  wa  zamani  wa  jeshi, Sultani Makenga , anaongoza  moja  kati  ya  batalioni.  Hakuna  msemaji wa  jeshi  alipatikana   kuthibitisha  mapigano  hayo  na  kundi  la M23. Omar Kavota, mkurugenzi wa  kituo  cha  kuhimiza  amani , demokrasia  na  haki  za  binadamu  amesema  Jumapili  kwamba vyanzo  katika  kijiji  cha  Ishasha  vimethibitisha  kuwapo  kwa wapiganaji  wa  kundi  la  M23  lakini  amesema "hakukuwa  na mapigano  ama  mapambano  bado".

Kongo M23 Rebellen M23-Kommandant Sultani Makenga
Sultani Makenga kamanda wa kundi la M23Picha: MICHELE SIBILONI/AFP/Getty Images

Hatari ya  mapigano

Majimbo  yenye  utajiri  mkubwa  wa  madini  nchini  Congo yameathirika  na  miaka  kadhaa  ya  mzozo  mbaya  kabisa, wakati mataifa  jirani  yakiunga  mkono  makundi  ya  waasi  katika  vita  vya wenyewe  kwa  wenyewe   dhidi  ya  mamlaka  ya  mjini  Kinshasa, na  sasa  wanamgambo  wanaotembea  hovyo  katika  eneo  hilo wanazusha  mapigano  makubwa  na  kuwatisha  raia.

Baada  ya  kushindwa  katika  mapigano  ya  mwaka  2013  na   jeshi la  Congo  na  majeshi  ya  Umoja  wa  mataifa , kundi  la  M23 lilikubali mpango  wa  kuweka  silaha  chini  na  kunyang'anywa silaha,  kuvunja  vikosi  vyao  na  kujumuishwa  katika   jamii  ya watu  wa  Congo.

Lakini  kurejea  kwa  waasi  hao  wa  zamani  kulikwama  , ambapo chini  ya  wapiganaji  200  kati  ya  wapiganaji karibu  1,900 waliokuwa  wakihifadhiwa  nchini  Uganda  na  13  kati  ya  mamia waliondoka  nchini  Rwanda  na  kurejea  Congo.

zum Thema - Friedensvertrag mit der M23 geplatzt - Kongo
Waziri wa mambo ya kigeni wa Uganda Henry Okello OryemPicha: Getty Images/Afp/Phil Moore

Wakati  wa  vita  vya  wenyewe  kwa  wenyewe  nchini  Congo maafisa  waliishutumu  Rwanda  na  Uganda  kwa  kuruhusu  waasi kutumia  ardhi  zao  kama  sehemu  ya  kuanzisha  mashambulizi yao. Hivi  karibuni  kabisa, wameyalaumu  mataifa  hayo  kwa  kuwa na  nia  mbaya  ya  kuwaruhusu wahalifu  kutembea  huru  kabisa , badala  ya  kuwarejesha  ili  kufikishwa  mahakamani  nchini  Congo.

Waziri  wa  mambo  ya  kigeni  wa  Uganda Henry Okello Oryem , akizungumza  na  shirika  la  habari  la  afp  mjini  Kampala , alikana vikali  kuwaunga  mkono  waasi  wa  M23  ambao  wamevuka mpaka.

Mwandishi: Sekione  Kitojo / afp

Mhariri: Idd Ssessanga