1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Waasi wa Libya wasaka misaada zaidi

21 Julai 2011

Waasi nchini Libya wameitaka Ufaransa kuipatia silaha zaidi kuweza kuwasaidia kuuvamia mji mkuu wa Libya, Tripoli katika kipindi cha siku chache zijazo, kabla ya kuanza mfungo wa mwezi wa Ramadhan.

https://p.dw.com/p/120kv
Mahmoud JibrilPicha: picture-alliance/dpa

Ombi hilo limetolewa na ujumbe wa waasi mjini Paris, ambalo limetoka kwa  kiongozi wa kijeshi kutoka katika mji wanaoushikilia wa Misrata kwenda kwa Rais wa Ufaransa Nicolas Sarkozy.

Rais Sarkozy alifanya mazungumzo jana katika makaazi yake na makanda wa waasi akiwemo Jenarali Ramadan Zarmuh, kanali Ahmed Hashem na kanali Brahim Betal Mal pamoja pia na mwakilishi kutoka katika mji wa Misrata ambao unashikiliwa na waasi Suleiman Fortia.

Sarkozy / Frankreich / Paris
Rais wa Ufaransa Nicolas SarkozyPicha: AP

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya mkutano wao huo, Suleiman Fortia alisema kwa msaada mdogo watakaoupata wataweza kuingia katika mji wa Tripoli, katika siku za karibuni.

Amesema wako nchini Ufaransa kwa ajili ya kujadiliana jinsi ya kufanya kazi hiyo.

Ufaransa imekuwa ikishiriki katika operesheni za kijeshi nchini Libya, kupitia uratibu wa mashambulio yanayofanywa na Jeshi la Kujihami la NATO dhidi ya jeshi lnaloongozwa na kiongozi wa nchi hiyo Muammar Gaddafi na pia lilikuwa taifa la kwanza la nje kulitambua Baraza la waasi la taifa la mpito.

Ufaransa tayari iliwapatia waasi wa Libya silaha kwa kuzidondosha kwenye milima ya Nafusa, kusini magharibi mwa mji mkuu wa nchi hiyo Tripoli ili kuwasaidia kujilinda na mashambulio yanayofanywa na majeshi ya Gaddafi.

Libyen Rebellen
Maeneo ya NafusaPicha: DW/Karlos Zurutuza

Vyanzo vya habari kutoka kwa waasi hao, vinasema kwamba wamekuwa wakitaka kutumia njia kama hiyo ya kuweza kufikishiwa silaha katika mji wa Misrata. Ambako pia lengo la ziara yao hiyo nchini Ufaransa ni kumfahamisha Rais Sarkozy kwamba uwezekano wa kuivamia Tripoli uko Misrata.

Lengo la waasi ni kuweza kumdhibiti Gaddafi kabla ya kuanza kwa mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhan ambao unatarajiwa kuanza Agosti mosi.

Wapiganaji waasi ambao wako magharibi mwa nchi hiyo wanasema wanasubiri amri ya kuweza kuanza mashambulio mapya kutokea katika milima ya Nafusa, kusini magharibi mwa mji mkuu wa Tripoli.

Wakati makamanda wa waasi wakiomba msaada wa silaha nchini Ufaransa, kiongozi wao Mahmoud Jibril anatazamia leo kutafuta msaada mwingine kuhusiana na operesheni yao hiyo ya kijeshi katika mazungumzo yake na Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje wa Hispania Trinidad Jimenez, mjini Madrid.

Wakati huohuo Ufaransa imekubali juu ya kiongozi wa Libya Muammar Gaddafi kubakia nchini mwake, iwapo atajitoa katika masuala ya siasa kulingana na makubaliano ya kusimamisha mapigano.

Lakini hata hivyo Marekani imesema ni juu ya Walibya wenyewe kuamua.

Wakati hayo yakitokea Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje wa Libya Abdelati al-Obeidi, yuko ziarani Urusi katika juhudi pia za kulipatia ufumbuzi tatizo la kisiasa nchini humo.

Mwandishi: Halima Nyanza

Mhariri: