1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Viongozi wa Ulaya kutoondoa haraka vizuizi vya Covid-19

26 Februari 2021

Viongozi wa Umoja wa Ulaya wamesema kuwa vizuizi vikali vya kusafiri vinapaswa kuendelea kutekelezwa wakati kanda hiyo ikapambana kuuweka sawa mpango wake wa kutoa chanjo ya virusi vya corona unaosuasua.

https://p.dw.com/p/3pwbv
EU-Gipfel Covid-19
Picha: Olivier Hoslet/AP Photo/picture alliance

Katika taarifa ya pamoja iliyotolewa baada ya mkutano wa kilele wa siku mbili ulioanza jana kwa njia ya video, viongozi 27 wa mataifa wanachama wa Umoja wa Ulaya wamesema hali ya janga la corona bado inatia wasiwasi na aina mpya ya virusi hivyo inaongeza mfadhaiko.

Wamekubaliana kuendelea na vizuizi vilivyopo huku wakizidisha kasi na kuimarisha mpango wa utoaji wa chanjo ambao unakwenda kwa mwendo wa konokono kutokana na uhaba wa chanjo uliopo.

Viongozi wakuu wa Umoja wa Ulaya wamewaambia Waandishi Habari kuwa itachukua miezi kadhaa kabla ya kanda hiyo kufikia uwezo wa kusambaza chanjo za kutosha za virusi vya corona.

Hata hivyo rais wa Halmashauri kuu ya Umoja wa huo Ursula von der Leyen amesema "Tunaamini kuwa tunaweza kufikia lengo letu la kutoa chanjo kwa asilimia 70 ya idadi ya watu wazima ifikapo mwishoni mwa majira ya kiangazi. Hao ni watu milioni 255 ndani ya Umoja wa Ulaya na tukiangalia takwimu zetu, hilo ni lengo tunaloweza kulifikia."

Umoja wa Ulaya huenda ukaanza kutoa vitambulisho kwa waliochanjwa 

Belgien EU Parlament Covid-19 Impfungen Ursula von der Leyen
Rais wa Halmashauri Kuu ya Umoja wa Ulaya, Ursula von der Leyen Picha: Francisco Seco/AP Photo/picture alliance

Umoja wa Ulaya pia unalenga kutayarisha mpango wa utoaji vitambulisho kwa watu waliopatiwa chanjo ya virusi vya corona kama njia ya kufungua tena shughuli za uchumi wakati wa msimu wa utalii utakapowadia majira ya kiangazi.

Pendekezo hilo linaungwa mkono kwa sehemu na viongozi wa mataifa wanachama wa Umoja wa Ulaya

Hata hivyo Von der Leyen amesema kutokana na sababu za kiufundi na maswali ya kisiasa yanayotaka majibu, mpango huo utahitaji kiasi miezi mitatu kabla ya kuanza kutekelezwa.

Serikali za mataifa wanachama wa Umoja wa Ulaya bado zinajadili iwapo iwaruhusu raia wake waliopatiwa chanjo ya Covid-19 kuhudhuria matamasha, kufanya safari za ndani na hata kula kwenye mikahawa kwa kutumia kitambulisho maalum.

Ulinzi na usalama kugubika siku ya pili ya mkutano

Belgien Brüssel | EU Gipfel | Merkel und Macron
Picha: Yves Herman/AP Photo/picture-alliance

Kwenye siku ya pili ya mkutano huo unaendelea leo Ijumaa viongozi wa Umoja wa Ulaya watazungumzia masuala ya Ulinzi na usalama na watamkaribisha katibu mkuu wa Jumuiya ya kujihami NATO Jens Stoltenberg kushiriki mazungumzo hayo.

Katika hatua nyingine Ufaransa na Ujerumani zimekubaliana kuwa wafanyakazi wote wanaovuka mpaka wa pamoja watalazimika kupimwa virusi vya coronaili kili uepusha uwezekano wa kufungwa kwa mpaka huo kama sehemu ya juhudi za kupunguza maambukizi.

Kansela Angela Merkel amewambia waandishi habari mjini Berlin, kuwa kufunga mipaka kwa nchi za Ulaya siyo kipaumbele hivi sasa lakini akaongeza kusema uamuzi wa kufunga mpaka kati ya Ujerumani, Austria na Jamhuri ya Czech lilikuwa suala tofauti.