1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Viongozi wa IGAD wazijadili Ethiopia, Kenya na Somalia

Yusra Buwayhid
21 Desemba 2020

Viongozi kutoka mataifa ya Afrika Mashariki ya Shirikisho la Maendeleo la Pembe ya Afrika IGAD, wamekutana Jumapili Djibouti kwa mkutano wa kilele, kujadili mzozo wa Tigray pamoja na mvutano kati ya Somalia na Kenya.

https://p.dw.com/p/3mzJX
Kongo Moussa Faki Mahamat Vorsitzenden der Kommission der Afrikanischen Union
Picha: Gislain Kusema/Press Office President DRC

Viongozi hao wamejadili mgogoro wa kibinadamu wa Ethiopia katika mkoa wake wa Tigray, pamoja na mvutano unaoongezeka kati ya mataifa jirani ya Kenya na Somalia.

Wawakilishi kutoka Djibouti, Ethiopia, Kenya, Uganda, Somalia na Sudan - wote wanachama wa IGAD - walikusanyika kwa mazungumzo kujadili "mchakato wa amani na usalama wa kanda,"amesema Waziri Mkuu wa Sudan Abdalla Hamsok kabla ya mkutano kuanza, kulingana na taarifa iliyotolewa na ikulu ya Kenya.

Soma zaidi: IGAD kufanya mkutano wa dharura kuhusu Tigray

Rais wa Djibouti Ismail Omar Guelleh, Uhuru Kenyatta wa Kenya, Mohamed Abdullahi wa Somalia Waziri Mkuu wa Sudan Abdalla Hamdok na Waziri Mkuu wa Ethiopia Abiy Ahmed wote walihudhuria mkutano huo.

Moussa Faki Mahamat, ambaye anaongoza Kamisheni ya Umoja wa Afrika nae pia alishiriki, na aliwahimiza wanachama wa IGAD kuisaidia Ethiopia kushughulikia mgogoro wa kibinadamu unaotokana na mzozo katika mkoa wake wa Tigray, kulingana na ikulu ya Kenya.

Soma zaidi: Misaada yawasili kwa mara ya kwanza katika jimbo la Tigray

Kufuatia mapigano ya Tigray kati ya vikosi vya serikali ya Abiy na chama cha People's Liberation Front (TPLF) jimbo hilo limetengeka na limekuwa vigumu kufikiwa. Umoja wa Mataifa unamshinikiza Abiy kuyaruhusu mashirika ya misaada kuwafikia raia wanaohitaji misaada ya kiutu.

Aidha Ofisi ya rais wa Sudan imesema Hamdok alikutana na Abiy pembezoni mwa kutano huo wa kilele huko Djibouti. Viongozi hao wamepanga kukutana tena Jumanne katika mji mkuu wa Sudan wa kujadili suala la mpaka unaoziunganisha nchi zao. Zaidi ya hayo, hakuna maelezo yaliotolewa.

Somalia na Kenya zatakiwa kufanya mazungumzo 

Wakati wa mkutano huo wa kilele, Faki pia alizitaka Kenya na Somalia kutuliza mvutano kupitia njia ya mazungumzo.

Bildcombo I Abiy Ahmed und  Uhuru Kenyatta
Abiy Ahmed (kulia) na Uhuru Kenyatta (kushoto)

Somalia ilivunja uhusiano wa kidiplomasia na Kenya mnamo Desemba 15, ikimshutumu jirani yake kwa kukiuka mipaka inayolinda uhuru wa taifa hilo.

Soma zaidi:Uhusiano wa kidiplomasia kati ya Somalia na Kenya mashakani

Kenya ni moja wapo ya wachangiaji wakubwa wa wanajeshi kwa ujumbe wa askari wa kulinda amani wa Umoja wa Mataifa AMISOM nchini Somalia, unaopambana na wanamgambo wenye itikadi kali wa kundi la Al-Shebab lenye mafungamano na Al-Qaeda.

Moja ya sababu za ugomvi kati ya Kenya na Somalia ni eneo la Jubaland, jimbo la kusini mwa Somalia linalopakana na Kenya.

Kenya inalitazama jimbo la Jubaland kama eneo linaloitenganisha ardhi yake na kundi la Al-Shebab, ikimuunga mkono kiongozi wa jimbo hilo Ahmed Madobe.

Vyanzo: (ap,afp)