1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Vilabu vya Bundesliga na tahadhari ya Ebola

17 Novemba 2014

Ugonjwa wa Ebola umewakosesha usingizi wakuu wa soka Afrika katika wiki za karibuni huku kukiwa na hali ya sintofahamu kuhusu Kombe la Afrika na sasa vilabu vya Bundesliga havijaacha kuchukua tahadhari

https://p.dw.com/p/1Dojp
Fußball Bundesliga 7. Spieltag Hertha BSC VfB Stuttgart 03.10.2014
Picha: Stuart Franklin/Bongarts/Getty Images

Borussia Dortmund walikuwa na wasiwasi kuhusiana na mchezaji wao Pierre-Emerick Aubameyang na wakamzuia kusafiri kuiwaikilisha Gabon ambayo ilitoka sifuri kwa sifuri na Angola.

Lakini wachezaji wengine sita wanaocheza kandanda lao hapa Ujerumani walipewa ruhusa na vilabu vyao ya kuzichezea nchi zao mwishoni mwa wiki. Nahodha wa timu ya taifa ya Guinea Ibrahima Traore aliisaidia timu yake kuizaba Togo mabao manne kwa moja. Klabu yake ya Borussia Moenchengladbach awali ilipendekeza kuwa wachezaji wake wasisafiri kwenda Afrika, lakini daktari wa timu Heribert Ditzel akasema kitisho cha maambukizi ya Ebola kilikuwa chini mno.

Kwanza kunakuwa na awamu ya uchunguzi ambapo Traore atafanyiwa vipimo kila siku kwa wiki tatu kabla ya kujiunga tena na klabu yake. Kama atakuwa na maumivu yoyote, basi atakaa nyumbani na kuchunguzwa kabla ya kurejea kikosini.

Cedric Makiadi wa Werder Bremen ataiwakilisha Congo katika mchuano dhidi ya Sierra Leone utakaochezwa nchini Cameroon kwa ajili ya kitisho cha Ebola. Mkurugenzi wa Sport wa Bremen Robin Schroder ameridhika na hatua maalum za tahadhari zilizochukuliwa kabla ya Makiadi kusafiri kwenda Afrika.

Salomon Kalou wa Hertha Berlin aliifungia mabao mawili Cote d'Ivoire dhidi ya Sierra Leone, wakati pia Salif Sane (Senegal na Hannover), Abdul Rahman Baba (Ghana na Augsburg) na Eric Maxim Choupo-Moting (Cameroon na Schalke) wakiwa dimbani mwishoni mwa wiki.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP/Rueters
Mhariri: Yusuf Saumu