1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

VFL Wolfsburg kutwaa ubingwa ?

18 Mei 2009

Finali jumamosi ijayo ama Wolfsburg au Munmich kuibuka bingwa.

https://p.dw.com/p/HskO

Nani atatoroka na kombe la ubingwa Jumamosi ijayo-Wolfsburg inayoongoza kwa pointi 2 au mabingwa Bayern munich wanaonyatia nafasi ya pili ?Manchester United,FC Barcelona na Inter milan tayari wametawazwa mabingwa katika Premier League, La Liga na Seria A:Mabingwa wa Tanzania Young Africans na mahasimu wao Simba wajiwinda kwa msimu ujao na mjamaica bingwa wa 0limpik na rekodi za dunia mita 100-200 na 100x4, Usain Bolt aweka rekodi nyengine -mara hii mita 150.

Ligi mashuhuri barani ulaya ambazo zimepamba moto kwani baadhi ya timu zimekwishatawaza mabingwa mwishoni mwa wiki na nyenginezo mwishoni mwa wiki ijayo.

Katika Bundesliga-kocha wa viongozi wa Ligi Wolfsburg iliopo usoni kwa pointi 2, hajaupokea mkono wa hongera aliopewa na mapema juzi Jumamosi kabla Wolfsburg kupambana na Werder Bremen katika fainali ya Bundesliga Jumamosi ijayo inayozikutanisha Wolfsburg na Bremen na mabingbwa Bayern Munich na Stuttgart:

Wolfsburg iliotamba na washambulizi wake 2-mbrazil Frafeti na Mbosnia ambao kwa pamoja wametia mabao 51 msimu huu, iliizaba Hannover mabao 5-0 kuhakikisha kwamba mwishoni huenda wingi wa magoli ukaamua wapi taji la ubingwa linaelekea-Wolfsburg au Munich.

Wolfsburg inahitaji kutoka sare tu na Bremen, Jumamosi ijayo ili kuvaa taji lake la kwanza kabisa wakati Munich iliopo pointi 2 nyuma lazima ishinde na kutaraji Wolfsburg inatiwa munda na Bremen.

Munich ilifanya madhambi makubwa Jumamosi ilipomudu sare tu ya mabao 2:2 kati yake na Hoffenheim. Hivyo, ilipoteza pointi 2 ilizohitaji sana kutwaa ubingwa Jumamosi ijayo bila kutegemea kuteleza kwa Wolfsburg.

Munich inahitaji kuilaza Stuttgart tena kwa si chini ya mabao 7, lakini kufanya hivyo itakua ni kama miujiza. Hasa kwa vile zote mbili zaweza kuibuka mabingwa iwapo mojawapo ikishinda na Wolfsburg ikiteleza mbele ya Bremen.

Wolfsburg inahitaji kutoka sare tu nyumbani Volkswagen Arena. Bremen ,ina kibarua kigumu keshokutwa Jumatano ikiwa na miadi na Shakhtar Donetsk ya Ukraine katika fainali ya Kombe la ulaya la UEFA.

Bremen huenda ikatolewa jasho na Waukraine na hivyo wakawa hoi, watakapoingia uwanjani na Wolfsburg Jumamosi. Kocha wa Wolfsburg, Felix Magath, ataiachamkono Wolfsburg ili kuiongoza Schalke msimu ujao.

Ndoto ya Hertha Berlin, timu ya jiji kuu Berlin, ndoto ya kutwaa ubingwa imetoweka baada ya kumudu sare 0:0 na Schalke. Hata hivyo, Berlin ina nafasi ya kucheza katika Champions League au kombe la ulaya la UEFA. Hamburg timu ya 4 iliokaribia kuvaa taji, ilichapwa bao 1:0 na FC Cologne. Armenia Bielefeld iliochapwa mabao 6-0 na Borussia Dortmund imemtimua kocha wake Michael Frontzeck.

Ama katika Premier League-ligi ya Uingereza, Manchester United imetwaa tena taji la ubingwa tena kwa mara ya 18 hapo Jumamosi waliponyakua pointi 1 waliohitaji kutoka Arsenal kufuatia sare ya 0:0. Arsenal, inayaotazamiwa sasa kumaliza nafasi ya 4 nyuma ya Liverpool na Chelsea, ilikaribia kutamba katika uwanja wa Man U huko Old Trafford. Kwa jumla ya pointi 87 huku mpambano mmoja ukisalia, Manchester United imetwaa kombe lake la 3 msimu huu kati ya 5 inayolenga kutwaa. Mei 27 Man U ina miadi na FC Barcelona katika finali ya kusisimua ya Champions League-kombe la klabu bingwa barani ulaya.

Huko Itali, mabingwa wapya ni wale wale wa zamani -Inter Milan. Inter imevaa taji na mapema huku mechi 3 zikisalia kukamilisha msimu wa Serie A. Kutawazwa tena kwa Inter Milan mabingwa kunafuatia pigo iliopata mahasimu wao AC Milan iliozabwa mabao 2-1 na UDINESE. Inter imepanga kusheherekea ushindi wao nyumbani Jumapili hii ijayo baada ya kupambana na Siena. Nahodha wa Inter Milan Paolo Maldini amepanga kustaafu msimu huu ukimalizika.

Katika La Liga, Ligi ya Spian, FC Barcelona inayotamba na Samuel Eto-o wa Kamerun na Lionel Messi wa Argentina, wametawazwa pia mabingwa na mapema baada ya mahasimu wao wakubwa Real Madrid kuteleza mbele ya Vilareal kwa kuchapwa mabao 3-2. Hata Barcelona ilizabwa mabao 2-1 na Mallorca.

Katika viwanja vya michezo nchini Kenya, mwanamichezo wetu Eric Ponda anaarifu:

Katika medani ya riadha, bingwa mara 3 wa olimpik na rekodi ya dunia, Mjamaica Usain Bolt, aliwika tena jana katika mbio za mita 150 mjini Manchester, Uingereza. Katika uwanja uliosheheni mvua, Usain Bolt hakujali na alitimka mbio kuweka rekodi ya masafa hayo kwa muda wake wa sekunde14.35 na hivyo kuivunja rekodi ya zamani ya sekunde14.8 iliowekwa na mtaliana Pietro Mennea hapo 1983.

Muandishi:Ramadhan Ali

Mhariri : J.Charo