1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uturuki kupata rais mpya

Jane Nyingi28 Agosti 2007

Bunge la Uturuki linatarajiwa leo kumchagua waziri wa mambo ya nje Abdullah Gul kuwa rais mpya baada ya mivutano ya miezi kadhaa.Hatua hiyo itaufanya wadhifa wa urais kwa mara ya kwanza katika historia ya uturuki kushikwa na mtu mwenye kufuata maadili ya kiislamu katika nchi isiyoegemea misingi ya kidini .

https://p.dw.com/p/CB1f
Abdullah Gül
Abdullah GülPicha: picture-alliance/dpa

Kuchaguliwa kwa Gul kuwa rais kutaifanya uturuki kuonekana imepiga hatua kubwa katika kuzingatia democrasia.Hata hivyo wachaganuzi wa kisiasa wanasema Gul anakabiliwa na kibarua kigumu katika uongozi wake,hasa ikizingatiwa itakuwa mara ya kwanza katika historia ya uturuki wadhifa huo kushikwa na mtu mwenye kufuata maadili ya kiislamu.

Chama tawala cha AKP chenye mizizi ya kiislamu hakitakuwa na wakati mgumu kumchagua Gul katika nafasi hiyo kwani kina wawakilishi 340 katika bunge lenye viti 550.Mshindi anatarajiwa kupata kura 276 katika duru hii ya tatu ya uchaguzi wa urais.

Gul mwenye umri wa miaka 56 aliposimama kwa mara ya kwanza mwezi aprili kuwania wadhifa huo, upinzani ulivuruga uchaguzi huo kwa kususia kwenda bungeni, huku jeshi,ambalo limepindua serikali nne tangu mwaka 1960 likitoa matamshi makali kwa serikali kuwa lipo tayari kuhakikisha kuwa taifa hilo halitawaliwi kwa misingi ya kidini.

Hali hiyo ilimfanya waziri mkuu Recep Tayyip Erdogen kuitisha uchaguzi mkuu wa mapema tarehe 22 mwezi julai ambapo chama tawala cha AKP kiliibuka mshindi na hivyo kupewa nafasi ya kumteua tena Gul.

Wapinzani wanasema chama cha AKP chenye mizizi ya kiislamu kina agenda ya siri ya kubadili maongozi ya sasa nchini Uturuki yasioendeshwa kwa misingi ya kidini na kuazishwa kwa maongozi ya taifa la iran.

Uturuki yenye wakaazi wapatao millioni 74 ni nchi ya yenye waislamu wengi lakini inaogozwa na katiba isiyoingiza dini katika maswala ya siasa.Chama tawala cha AKP kinatuhumiwa kuwa kinajaribu kupuuza utaratibu huo wa kutenganisha dini na siasa,utaratibu amabo uliazishwa baada ya kuporomoka kwa ufalame wa Ottoman na ikaundwa jamuhuri mpya ya uturuki.