1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Utawala kuwafutia mashtaka waandamanaji Myanmar

6 Agosti 2021

Utawala wa jeshi wa Myanmar umejitolea kuwafutia mashtaka waandamanaji waliohusika katika maandamano au mgomo ikiwa watajitokeza.

https://p.dw.com/p/3ye9X
Proteste in Myanmar
Picha: AP/picture alliance

Katika taarifa iliyotolewa kupitia vyombo vya habari vya serikali, wale wanaotaka kurudi nyumbani kwa hiari yao wanaweza kuwasiliana kupitia nambari za simu zilizotolewa au kujiwasilisha katika vituo vya polisi karibu nao, au hata kwa usimamizi wa serikali za wilaya na miji. Soma Jeshi Myanmar lajiongezea miaka miwili madarakani

Taifa hilo la Asia ya Kusini limekuwa katika machafuko tangu jeshi lilipoipindua serikali iliyochaguliwa kidemokrasia ya Aung San Suu Kyi miezi sita iliyopita, na kusababisha wimbi la maandamano na harakati za kutotii utawala ambazo zimepooza shughuli za kawaida katika baadi ya maeneo nchini humo. Soma Myanmar yaanza kuwaachilia huru wafungwa wengine 2,300

Kina nani hawatasamehewa?

Weltspiegel 06.07.2021 Myanmar Protest
Maandamano MyanmarPicha: ASSOCIATED PRESS/picture alliance

Kulingana kundi la wanaharakati la Chama cha msaada kwa Wafungwa wa Kisiasa, tangu mapinduzi yalipoanza, vikosi vya usalama vimewakamata zaidi ya watu 7,000, huku wengine 1,984 wanatafutwa.

Hata hivyo, chombo cha habari kinachoendeshwa na serikali cha Global New Light kimeripoti kuwa hakuna msamaha utakaotolewa kwa mtu yeyote anayetafutwa kwa uhalifu kama mauaji, kuchoma moto au kushambulia wanajeshi, huku kikilaumu uchochezi kutoka kwa wanachama wa chama cha Suu Kyi.

Min Aung Hlaing
Min Aung HlaingPicha: AP/picture alliance

Mtawala wa jeshi la Myanmar, Min Aung Hlaing, wiki hii aliahidi kufanya uchaguzi ifikapo Agosti 2023.

WFP haina fedha za kutosha

Huku hayo yakijiri shirika la Mpango wa Chakula Ulimwenguni, WFP, limeonya kwamba huenda lisiwe na uwezo wa kifedha wa kutosha kwa miezi sita ijayo kusaidia mamilioni ya watu nchini Myanmar wanaokabiliwa na ukosefu wa usalama wa chakula wakati wimbi la maambukizo ya COVID-19 na machafuko ya kisiasa katika taifa hilo la kusini mashariki mwa Asia yakiendelea. Soma Umoja wa Mataifa waonya juu ya kitisho cha njaa Myanmar

Katika taarifa yake, WFP imesema inahitaji dola milioni 86 ili kusaidia katika kupambana na baa la njaa nchini humo. Mkurugenzi wa shirika hilo nchini Myamanr Stephan Anderson amesema baa la njaa linaendelea kuenena.

Aidha Shirika hilo la msaada wa binadamu linakadiria watu milioni 6.3 nchini Myanmar wanaweza kukabiliwa na uhaba wa chakula katika miezi sita ijayo, kutoka milioni 2.8 kabla ya mapinduzi ya jeshi ya mwezi Februari.

 

Vyanzo; (Reuters)