1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ushindi wa Macron utabainika baada ya miaka 5

John Juma
19 Juni 2017

Kambi ya Emmanuel Macron imesema ushindi halisi wa Macron utabainika baada ya miaka mitano wakati ambapo mageuzi kadhaa yatakuwa yamefanywa.

https://p.dw.com/p/2extn
Frankreich Präsident Macron
Picha: picture-alliance/abaca/L. Christian

Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron ameahidi kubadilisha hali ya siasa ya nchi hiyo baada ya chama chake kushinda viti vingi vya ubunge hali inayomwezesha kufanya mageuzi makuu aliyoyataka kuleta maendeleo. Hata hivyo kambi ya Macron inasema ushindi kamili utabainika baada ya miaka mitano.

Chama cha Emmanuel Macron ambacho ni cha mrengo wa wastani-Republic on The Move (LREM) na mshirika wake wa mrengo wa wastani unaoegemea kulia Modem, vilishinda viti 350 katika jumla ya viti 577 vya bunge la taifa, katika duru ya pili ya uchaguzi ambayo wapiga kura wachache ndio walijitokeza.

Msemaji wa serikali Christophe Castaner alisema kwa zaidi ya asilimia 50 ya wapiga kura kutojitokeza ni pigo kwa wanasiasa huku akiongeza kuwa ipo haja ya kubadilisha siasa za Ufaransa.

Hata hivyo Castaner ameiambia radio RTL kuwa ushindi kamili si ule uliopatikana kupitia uchaguzi wa wabunge, bali ushindi kamili utabainika baada ya miaka mitano wakati ambapo watakuwa wameshafanya mageuzi mbalimbali.

Japo chama kipya cha Macron hakikupata ushindi jinsi ulivyobashiriwa na kura za maoni, kilipata viti vingi na kuviaibisha vyama vikuu vya tangu jadi vya Conservative na Republican ambavyo ndivyo vimekuwa vikipokezana madaraka kwa miongo mingi.

Wawekezaji wauunga mkono ushindi wa Macron

Emmanuel Macron und Francois Bayrou
Picha: Picture alliance/dpa/I. Kalashnikova/Sputnik

Wawekezaji wamepokea na kuukubali ushindi wa Macron. "Baada ya mageuzi tunayotarajia Macron kutekeleza, Ufaransa inaweza kuwa taifa lenye uchumi thabiti zaidi miongoni mwa nchi za Umoja wa Ulaya katika kipindi cha mwongo mmoja ujao, na kupiku Ujerumani ambayo kujitenga kwa Uingereza na Umoja wa Ulaya kunalemaza mipango yake ya maendeleo ya muda mrefu.” Amesema Holger Schmieding ambaye ni mwanauchumi mkuu katika benki ya Ujerumani ya Berenberg.

Kwa haraka, Macron anataka kulegeza sheria za ajira kabla ya kugeuza sheria za malipo ya pensheni mwaka ujao. Wakati wa kampeni, Macron pia aliahidi kupunguza kodi kwa mashirika kutoka asilimia 33 hadi 25 kando na kuwekeza bilioni 50 za fedha kwenye sekta ya nishati, elimu na miundo mbinu ya uchukuzi.

Hata hivyo, Macron atahitaji kuwazia upungufu wa bajeti ya Ufaransa. Benki ya Ufaransa imebashiri kuwa kwa mara nyingine upungufu huo utakiuka kipengee cha Umoja wa Ulaya cha asilimia tatu ya jumla ya mapato ya kila mwaka.

"Ni kwa manufaa ya Ufaransa, kwa udhibiti wake kisiasa na kiuchumi ili kuenda sambamba na malengo yake."  Amesema Pierre Moscovici ambaye ni kamishna wa uchumi na masuala ya fedha wa Ufaransa alipozungumza na shirika la habari la runinga ya Public Senat.

Changamoto kutoka kwa waliosusia kura

Frankreich Wahl 2017 |
Picha: picture alliance/AP Photo/C. Paris

Kwamba watu wengi hawakujitokeza kupiga kura, inamaanisha Macron atahitaji kumakinika mno na mageuzi katika nchi ambayo ina vyama thabiti vya biashara na pia historia ya maandamano ambayo yamelazimisha baadhi ya serikali kulegeza baadhi ya sheria.

Aliposhinda urais mnamo mwezi Mei, Macron alijaza pengo la kisiasa lililotokana na mpagaranyiko kati ya chama cha kisosholiti na Republican, na ushindi wa viti vya ubunge umekamilisha kile ambacho kilionekana kutowezekana mwaka mmoja uliopita.

Warepublican na washirika wake wa Conservative wana viti 131 na wataunda kundi kubwa la upinzani bungeni. Chama chenye sera kali za mrengo wa kulia Front kilishinda viti vinane huku chama cha kisosholisti kikipata viti 44, hiyo ikiwa idadi ya chini zaidi ya viti kwa chama hicho kwa miongo kadhaa.

Katika uchaguzi huo wa Jumapili, wanawake wengi walichaguliwa kuliko uchaguzi wowote ule, hiyo ilitokana na uamuzi wa Macron kwamba kuwe na usawa wa kijinsia kati ya waliogombea viti vya bunge kutumia chama chake.

Mwandishi: John Juma/RTRE

Mhariri: Josephat Charo