1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Upinzani nchini DRC walaani ukandamizaji wa polisi

Admin.WagnerD1 Julai 2019

Upande wa upinzani nchini Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo umelalamika juu ya matumizi ya nguvu yaliyofanywa na polisi wakati wa mandamano yao mjini Goma siku ya Jumapili ambapo mtu mmoja aliuwawa.

https://p.dw.com/p/3LOZB
DRK Protest in Goma, Ostkongo
Picha: DW/J. Vagheni

Hayo yanakuja wakati rais Felix Tshisekedi akiwatolea mwito raia wa jimbo la Ituri waliojiunga na makundi ya wapiganaji kuweka chini silaha ilikuchangia kwenye maendeleo ya taifa.

Tshisekedi ameyasema hayo mjini Bunia alikokwenda  jana kwa ziara ya kikazi ya kutathmini  hali ya kiusalama. 

Akiwahutubia wakaazi wa mji huo wa Bunia kwenye mkutano wa hadhara siku ya Jumapili, rais Felix Tshisekedi amesema kwamba atafanya kila awezalo ili kumaliza machafuko kwenye mitaa ya Djugu na Mahagi, jimboni humo.

Amewatolea pia wito raia wa jimbo hilo la Ituri kusitisha umwagikaji wa damu na kukuza amani na maridhiano.

"Ninawaletea ujumbe wa amani na upendo. Wale waliochukuwa silaha, ninawambia hivi ikiwa wataacha vita na chuki. Tutafanya kila tuwezalo ili kuwaletea wajasiriamali wengi kwenye jimbo hili. Tutaunda ajira kwa vijana na kujenga barabara ili kwa pamoja tujenge nchi yetu" amesema Tshisekedi wakati wa hotuba yake.

Rais Tshisekedi kuzuru pia kambi za wakimbizi 

Sambia Felix Tshisekedi, Präsident des Kongo
Picha: Kongo Presidency/G. Kusema

Baadae Jumatatu rais Tshisekedi anatarajiwa kuzuru kambi za wakimbizi wa vita kutoka kwenye mitaa ya Djugu na Mahagi ambao ni zaidi ya laki tatu ambapo ananuwia kutoa wito wa kuwa kurejea kwenye maeneo yao ya vijiji.

Mara baada ya kuwasili kwake mjini Bunia, rais Tshisekedi aliongoza kikao cha kamati ya usalama ili kutathmini hali ya kiusalama.

Meja Jerry Gbelo,msemaji wa jeshi aliyehudhuria kikao hicho amesema kwamba jeshi tayari limefanikiwa kuwaondoa wapiganji kwenye vijiji kadhaa.

"Siku chache zilizopita hali ilikuwa tete kwenye mitaa ya Djugu na Mahagi ambao mauwaji na visa vya ukatili vilifanywa na wapiganaji wanaongozwa na Ndudjolo na kusababisha maelfu ya raia kuhayama makazi yao. Kwa siku ya leo jeshi limethibiti maeneo hayo na kiongozi wa kundi hilo la wapiganaji hajulikani aliko." alisema Jenerali huyo.

Tshisekedi ametarajiwa pia kukutana na viongozi wa mashirika ya kiraia kikao kitakachofuatiwa na mkutano na waandishi habari wa kitaifa.

Upinzani wasema polisi inatumia nguvu kubwa

Proteste im Kongo
Picha: Getty Images/AFP/J. Wessels

Wakati huohuo upinzani umetuhumu polisi na utawala wa Felix Tshisekedi kwa kuwanyayasa waandamanaji. Polisi walitawanya waandamanaji hao kwa kutumia gesi ya kutoa machozi  mjini Kinshasa na Goma.

Martin Fayulu kiongozi wa upinzani alizuiliwa kushiriki maandamano hayo na polisi walitoboa magurudumu yote ya gari lake.

"Jana Tshisekedi alikuwa akiandamana nasi kwenye upinzani. Tulikuwa tukilaani kile Kabila alikuwa akitufanyia pamoja lakini leo yeye pia maechukuwa mwenendo huohuo wa Kabila.Mungu ni mkubwa ,raia wanaonyesha ujasiri wao kwa kuandamana kuomba ukweli wa uchaguzi."

Polisi imelezea kwamba mtu mmoja alifariki jana mjini Goma kufuatia mandamano hayo.

Juni 30 ambayo huwa ni siku ya maadhimisho ya siku ya uhuru wa Congo, upinzani uliitisha maandamano ili kupinga uamuzi wa mahakama ya katiba uliobatilisha uchaguzi wa wabunge 23 na maseneta wawili wa upinzani.