UN yaonya kwamba Sudan Kusini imo katika mgogoro mbaya
11 Februari 2026
Mkuu wa ulinzi wa amani wa Umoja wa Mataifa Jean-Pierre Lacroix amesema mvutano wa kisiasa nchini Sudan Kusini unazidi kuongezeka, kusababisha ghasia na kuliweka taifa hilo changa duniani katika hali mbaya zaidi.
Mkuu huyo ametoa mwito kwa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa na jumuiya ya kimataifa kuhakikisha kwamba serikali ya Sudan Kusini na upinzani wanarejea kwenye meza ya mazungumzo na kutafuta suluhu.
Ikumbukwe kwamba mvutano huo mkubwa nchini Sudan Kusini ulianza mnamo Machi 2025, wakati wanamgambo wa Nuer walipoteka ngome ya jeshi. Serikali ya rais Salva Kiir ikajibu kwa kumshtaki makamu wa rais Rieck Machar na viongozi wengine wa upinzani kwa uhaini, mauaji, ugaidi na uhalifu mwingine lakini pia kumsimamisha kazi makamu wa rais.
Kesi hiyo ya uhaini imekuwa ikiendelea tangu mwishoni mwa 2025.