1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

UN yaliambia jeshi la Myanmar liwache kuwauwa waandamanaji

Saleh Mwanamilongo
4 Machi 2021

Mkuu wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Haki za Binaadamu Michelle Bachelet amelitaka jeshi nchini Myanamar kusisitsha mauwaji na kuwakamata waandamanaji nchini humo.

https://p.dw.com/p/3qDYO
Michelle Bachelet | UN Hochkommissarin für Menschenrechte
Picha: picture-alliance/Keystone/S. Di Nolfi

Mkuu wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Haki za Binaadamu Michelle Bachelet amelitaka jeshi nchini Myanamar kusisitsha mauwaji na kuwakamata waandamanaji nchini humo. Amesema zaidi ya watu 54 wameuliwa na polisi na jeshi tangu mapinduzi ya kijeshi yalipofanyika. Wakati huo huo maandamano mengine mapya yamezuka leo mjini Yangon. 

Kwenye taarifa iliyotolewa leo mjini Geneva, mkuu wa ofisi ya Umoja wa Mataifa ya haki za Binadamu ameelezea kuhuzunishwa kwake na mauwaji ya waandamanaji pamoja na mashambulizi dhidi ya wahudumu wa afya na magari ya kubeba wagonjwa yanayojitokeza kuwatibu majeruhi. Michelle Bachelet amelitaka jeshi kusitisha haraka mauwaji hayo.

Myanmar | Proteste nach Militärputsch
Picha: STR/AFP/Getty Images

Bachelet amesema katika taarifa kuwa wahanga na manusura wa matukio hayo ni sharti wasinyimwe haki ya kujua ukweli na kuwawajibisha waliohusika. Bachelet ameelezea hofu yake kuwa huenda ukiukaji huo ukaendelea bila kufanywa uchunguzi wa nje.

China yapinga uingiliaji kati wa masuala ya ndani

 Msemaji wa wiraza ya mambo ya nje wa China,Wang Wenbin ametoa mwito kwa pande zote kujizuwiya na machafuko zaidi.

'' China inawasiliana na pande zote nchini Myanmar na inapendekeza kupunguza hali ya uhasama. Tunaunga mkono nchi za kusini mashariki mwa Asia, ASEAN, katika kutafuta suluhisho la maridhiano na kutoingilia kati masuala ya ndani ya nchi wanachama.''

Miongoni mwa watu 54 waliouliwa tangu kufanyika mapinduzi ya kijeshi, 38 waliuliwa Jumatano pekee katika mandamano kwenye miji kadhaa ya Myanmar. Karibu watu 700 walikamatwa jana pekee huku wengi wao wakichukuliwa katika kamatakamata ya jeshi na polisi ya nyumba hadi nyumba. Kwa jumla watu 1.700 wamekamatwa tangu Februari mosi.

Jeshi na polisi wa Myanmar vyatuhumiwa na Umoja wa Mataifa kuhusika na mauwaji ya waandamanaji.
Jeshi na polisi wa Myanmar vyatuhumiwa na Umoja wa Mataifa kuhusika na mauwaji ya waandamanaji.Picha: REUTERS

Miongoni mwa waliokamatwa ni pamoja na wabunge,wanaharakati wa siasa, waandishi habari, waalimu,wahudumu wa afya, wafanyakazi wa umma na mapadri.

 Ofisi ya haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa imehisi kwamba idadi ya waliokamatwa pia ni kubwa zaidi. Maandamano yamefanyika kwenye maeneo zaidi ya mia tano.

Umoja wa Ulaya wasitisha misaada yake 

 Waandamanaji walijitokeza tena leo Alhamisi,huku wengi wao wakiwa na hofu kufuatia mauwaji ya hapo jana. Watu walioshuhudia wamesema polisi walitumia gesi ya kutoa machozi kuwatawanya waandamanaji hao. Kwenye mtaa wa San Chaung mjini Yangon, kitovu cha maandamano hayo, bango la picha ya kiongozi wa mapinduzi hayo ya kijeshi, Min Aung Hlaing, liliangushwa na kukanyagwa na waandamanaji.

Wakati huo huo, Umoja wa Ulaya umesitisha miradi yote ya maendeleo nchini Myanmar ili kuepusha msaada wa kifedha kwa jeshi baada ya kukamata madaraka mwezi uliopita. Halmashauri Kuu ya Umoja wa Ulaya imethibitisha kuwa imesitisha msaada wa kifedha, ambao katika miaka iliyopita ulihusisha zaidi ya euro milioni 200 katika mipango tofauti inayotekelezwa kwa miaka minne.