1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Umoja wa Mataifa wamuunga mkono Ouattara.

Halima Nyanza9 Desemba 2010

Baraza la Usalama la Umoja wa mataifa limetoa taarifa ya kumuunga mkono kiongozi wa upinzani nchini Cote d'Ivore Alassane Ouattara kuwa ndiyo mshindi wa uchaguzi wa Rais uliofanyika nchini humo Novemba 28.

https://p.dw.com/p/QTuF
Kiongozi wa upinzani wa Cote d'Ivoire Alassane Ouattara.Picha: AP

Wanachama 15 wa baraza hilo la usalama la Umoja wa Mataifa  pia wameonya kwamba baraza hilo liko tayari kuweka vikwazo dhidi ya mtu yoyote ambaye atajaribu kuvuruga mchakato wa amani ama kuzuia  operesheni za Umoja wa Mataifa nchini Cote d'Ivoire.

Aidha baraza hilo pia limetoa wito wa pande zote kuheshimu ushindi alioupata kiongozi huyo wa upinzani nchini humo Alassane Ouattara, kufuatia uchaguzi wa rais uliofanyika nchini humo mwezi uliopita.

Baraza la Usalama pia limemuongezea shinikizo Rais anayemaliza muda wake Laurent Gbagbo kuachana na madai yake ya kuongoza nchi hiyo ya Afrika magharibi.

Katika taarifa iliyosomwa na mjumbe wa Marekani katika baraza hilo Brooke Anderson, ambaye nchi yake kwa sasa ndiyo inashikilia nafasi ya Urais, baraza hilo limesema linalaani juhudi zozote zitakazovuruga matakwa ya watu ama kuhujumu uaminifu wa zoezi hilo la uchaguzi.

Makubaliano yaliyofikiwa katika taarifa hiyo ambayo yalikuwa yamekawizwa toka Ijumaa iliyopita na Urusi, baada ya kudai kwamba Umoja wa Mataifa  haupaswi kuwa katika nafasi ya kuamua nani kashinda katika uchaguzi huo.

Hata hivyo nchini za magharibi zimesema kuwa mjumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Cote d'Ivore Y.J.Chio na haki ya kutangaza ushindi wa Alassane Ouattara, kwa sababu amepewa mamlaka ya kuthibitisha matokeo ya uchaguzi, kulingana na makubaliano ya amani yaliyofikiwa mwaka 2005, kufuatia vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyotokea mwaka 2002 na 2003.

Tume ya uchaguzi nchini Cote d'Ivoire ilimtangaza mshindi kiongozi huyo wa upinzani Alassane Ouattara, lakini  baraza la katiba nchini humo linaloongozwa na mshirika wa Bwana Gbagbo lilipindua matokeo hayo kwa madai ya kufanyika udanganyifu katika baadhi ya maeneo na kumtangaza Gbagbo kuwa mshindi.

Lakini licha ya miito mbalimbali kutolewa ya kumtaka kuachia madaraka, ikiwemo kutoka katika Jumuia ya Kiuchumi ya Nchi za Afrika magharibi -ECOWAS- Umoja wa Ulaya na Marekani, bado bwana Gbagbo amekataa kufanya hivyo.

Aidha rais huyo anayemaliza muda wake ameendelea kuwa na udhibiti katika jeshi na televisheni ya taifa.

Mwandishi: Halima nyanza(afp, reuters)

Mhariri:Mtullya Abdu