1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Umoja wa mataifa hauna mamlaka Sudan -Bashir

10 Mei 2012

Wakati kukiendelea kushuhudiwa mapigano katika mpaka kati ya Sudan na Sudan Kusini, Rais wa Sudan Omar al Bashir amesema si Umoja wa Mataifa wala Umoja wa Afrika wana mamlaka ya kuipangia la kufanya.

https://p.dw.com/p/14sr3
Rais wa Sudan Omar al Bashir
Rais wa Sudan Omar al BashirPicha: Reuters

Matamshi hayo yanakuja baada ya Azimio la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lililoketi Mei 2 mwaka huu na kuzitaka Sudan na Sudan Kusini kusitisha mapigano katika mgogoro wa eneo hilo uliojitokeza baada ya Sudan Kusini kujitenga na kuwa huru julai mwaka jana.

Kiongozi huyo wa Sudan amesema haya wakati mapigano yakiendelea katika mpaka huo na Sudan Kusini ambapo utawala wa Rais Salva Kiir unasema mapigano yanatokana na kurejea tena mashambulio ya angani kutoka ndege za Sudan.

Azimo la Umoja wa Mataifa limezitaka pande zote mbili kuondoa majeshi yao mpakani lakini Sudan imesema haitoweza kufanya hivyo mpaka kutakapokuwepo na maridhiano ya mipaka baina yao.

Rais Omar el Bashir na Rais Salva Kiir
Rais Omar al Bashir na Rais Salva KiirPicha: picture-alliance/dpa

Hali katika eneo hili hapo awali ilikuwa ya mashaka wakati ambapo Sudan Kusini ilipoteka mji wenye utajiri wa mafuta wa mpakani wa Heglig ukidai kuwa ni eneo lake mara baada ya kuumiliki kwa siku10.

Baadae Sudan ilidai kuwa imeukomboa mji huo baada ya kuwashambulia na kuwafurusha askari wa Sudan Kusini.

Umoja wa mataifa umetadharisha mapema kuwa kama hali inaendelea kuwa hivyo bila ya kufikia muafaka basi mwisho ulikuwa ni Ijumaa iliyopita baada ya hapo mataifa haya mawili yaliyodumu katika vita vya wenyewe kwa wenyewe kwa miaka 21 yajiandae na vikwazo.

Kabla ya kauli hii ya Rais Bashir, majeshi ya Sudan yamesema yaliwafurusha Askari wa Sudan Kusini katika miji ya Kafia Kingi na Kafindibei upande wa Darful Kusini.

Huku danadana ya matamshi ikiamia kwa Sudan Kusini, msemaji wa taifa hilo Kella Kueth amesema kumekuwepo na mashambulio mengi katika maeneo yao ambayo yameratibiwa na Sudan.

Matamshi ya sasa ya Rais Bashir yanapingana kauli ya taifa hilo ya kuheshimu makubaliano ya kusitisha mapigano lakini walisema bayana kuwa kama Sudan Kusini ikiendeleza vitendo vyake vya kuteka na kushambulio nchi yao wao watakachokifanya ni kujibu mashambulizi tu kwa nia ya kujilinda.

Rais Bashir amewahi kuihita Serikali ya Juba kuwa wadudu na wakitakiwa kuondolewa kabisa. Alituhumu kuwa SPLA wana nia ya kuupindua utawala wake na kusema kama watafanya hivyo na wao hawatasalimika.

Eneo la Heglig baada ya mapigano
Eneo la Heglig baada ya mapiganoPicha: Reuters

Rais Bashir ametamka wazi kuwa kama suala la usalama halitashughulikiwa kwanza basi wao hawataketi tena kuzungumzia mambo mengine ya kutatua mgogoro baina yao na Sudan Kusini.

Mwandishi: Adeladius Makwega

Mhariri: Yusuf Saumu