1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ulimwengu unaadhimisha Siku ya Wanawake

8 Machi 2016

Leo tarehe 8 Machi ni siku ya wanawake duniani. Wanawake katika mataifa zaidi ya 90 bado wanakosa haki sawa ya kumiliki ardhi, hali ambayo pia inaonekana kukamwisha uzalishaji wa mazao ya chakula

https://p.dw.com/p/1I94o
Wanawake wakijishughulisha na kilimo nchini Burundi.
Wanawake wakijishughulisha na kilimo nchini Burundi.Picha: picture alliance/africamediaonline

Mataifa Mashariki na Kusini mwa Afrika tayari yameboresha sheria zao ili kuruhusu wanawake waweze kumiliki ardhi kirahisi kwa ajili ya shughuli za kilimo. Alisema Kalibata.

" Barani Afrika , wanawake sita kati ya kumi wanategemea ardhi kwa jili ya kuendesha maisha yao ya kila siku." alisema Kalibata alipozungumza na shirika la Thompson Reuters Foundation ikiwa ni katika kuelekea maadhimisho ya siku ya wanawake duniani.

Aliongeza kuwa iwapo tunataka kuwa na maendeleo ya kweli duniani basi wanawake wanapaswa kuwa miongoni mwa wanaomiliki njia kuu za uzalishaji. Asilimia 30 ya wanawake wanamiliki ardhi Mashariki na Kusini mwa Afrika

Kiasi cha asilimia 30 ya wanawake wanamiliki ardhi Mashariki na Kusini mwa Afrika ukilinganisha na Afrika ya Kaskazini na Afrika ya Kati ambako ni asilimia chini ya kumi ya wanawake ambao wanamiliki ardhi.

Wanawake mashambani
Wanawake mashambaniPicha: picture-alliance/Ton Koene

Wanawake wanapokosa haki ya kumiliki ardhi basi wanakuwa na wakati mgumu wa kutoa huduma ya chakula na elimu kwa watoto wao.

Sekta ya uzalishaji kupitia katika kilimo nayo pia inaathirika na hivyo kusababisha ugumu katika kuwalisha kiasi cha watu milioni 795 duniani kote wanaokabiliwa na njaa.

Wanawake nchini Rwanda wanamiliki nusu ya sehemu ya ardhi katika familia

Wakati wa kipindi chake kama waziri wa kilimo nchini Rwanda ambacho kilimalizika mnamo mwaka 2014, Kalibata alisaidia kuleta mageuzi kadhaa katika sheria ambayo yaliwezesha mwanamke kumiliki nusu ya sehemu ya ardhi ambayo inamilikiwa na familia.

Katika mataifa mengi yanayoendelea, hati ya umiliki wa ardhi inakuwa na jina la mwanaume pekee. Waziri huyo alifanikisha pia wanawake wajane kumiliki aridhi ndani ya familia pindi waume zao wanapofariki dunia.

Wanawake wakiwa katika harakati za kilimo barani Afrika
Wanawake wakiwa katika harakati za kilimo barani AfrikaPicha: AP

" Ama kwa hakika mambo yanakwenda vizuri nchini Rwanda hasa linapokuja swala la haki ya wanawake katika umiliki wa aridhi" alisema Rena Singer, ambaye ni msemaji wa taasisi ya kupigania haki yenye makao yake makuu jijini Washington Marekani.

"Kama wanawake hawamiliki aridhi, tunashuhudia kuendelea kwa kukosekana usawa wa kijinsia. Njia pekee ya watu wengi walio masikini katika jamii kuweza kuendesha maisha yao ni kuwa na uwezo wa kumiliki aridhi kwani wanakuwa hawana uwezo kifedha kununua aridhi.

Hata katika mataifa kama Rwanda ambako kuna sheria nzuri za umiliki wa aridhi mapungufu yaliyopo katika kusimamia utekelezaji wa sheria hizo nikiwa ni pamoja na mfumo dume yanakuwa kikwazo kwa wanawake kumiliki ardhi kwa ajili ya shughuli za kilimo. Alisema Kalibata.

Serikali inapaswa kuwekeza katika kutoa elimu juu ya umiliki wa ardhi.

Serikali inapaswa kuwekeza katika kutoa elimu kwa jamii ili wanawake wengi wapate elimu ya kutosha kuhusiana na haki yao ya kumiliki aridhi, kwani walio wengi hawana ufahamu juu ya haki hiyo.

Takwimu kutoka katika Shirika la Umoja wa Mataifa linalohusika na masuala ya kilimo zinaonyesha kuwa wanawake wanamiliki chini ya robo ya aridhi katika mataifa yanayoendelea.

Mwandishi: Isaac Gamba/ RTRE
Mhariri : Mohammed Abdul-Rahman