1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ukraine yasema mazungumzo na Urusi huenda yakasambaratika

30 Aprili 2022

Rais wa Ukraine Volodymr Zelensky amesema mazungumzo na Urusi yanaweza kusimamishwa kabisa kutokana na ukatili unaotendwa na majeshi ya Urusi.

https://p.dw.com/p/4AeHX
Ukraine-Konflikt - Selenskyj in Kiew
Picha: Uncredited/Ukrainian Presidential Press Office/AP/picture-alliance

Wajumbe wa Ukraine na Urusi mpaka sasa wameshafanya duru kadhaa za mazungumzo ikiwa pamoja na yale ya ngazi ya juu yaliyofanyika nchini Belarus na Uturuki ambapo hatua thabiti hazikupigwa. Waziri wa mambo ya nje wa Urusi Sergei Lavrov ameiambia televisheni ya  Al Arabia kuwa Ukraine inabeba lawama kwa kukwama kwa mazungumzo hayo na ameeleza kuwa Ukraine inaendelea kubadilisha msimamo wake kwa kufuata maagizo ya Marekani na Uingereza.

Wanajeshi wa Ukraine wakipokea mafunzo karibu na mji wa Kharkiv
Wanajeshi wa Ukraine wakipokea mafunzo karibu na mji wa KharkivPicha: Andrew Marienko/AP Photo/picture alliance

Urusi imesema haimo katika vita na nchi za NATO. Waziri wa mambo ya nje wa Urusi Sergei Lavrov ameliambia shirika la habari la RIA kuwa Urusi haimtishii yeyote kwa vita vya nyuklia bali amezilaumu nchi za magharibi kwa kufanya hivyo. Amesema hali kama hiyo itaongeza hatari ya kuzuka vita vya nyuklia. Huku hayo yakiendelea mji mkuu wa pili wa Ukraine wa Kharkiv umekumbwa na mashambulizi ya makombora wakati ambapo Urusi ikiendelea na mashambulizi yake nchini humo.

Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky amesema vikosi vyake vinapambana kwa mafanikio katika eneo hilo. Rais wa Ukraine pia amesema Urusi inataka kuliteketeza kabisa eneo la Donbas na kwamba mashambulizi ya Urusi katika eneo hilo la mashariki yanaifanya Donbas kuwa ni sehemu isiyoweza kukalika.

Vira Hyrych ripota wa radio Free Europe aliyeuawa baada ya majeshi ya Urusi kufanya mashambulio katika mji mkuu wa Ukraine.
Vira Hyrych ripota wa radio Free Europe aliyeuawa baada ya majeshi ya Urusi kufanya mashambulio katika mji mkuu wa Ukraine. Picha: RFE/RL’s Ukrainian Service

Katika kadhia nyingine ripota wa radio Free Europe amekufa baada ya majeshi ya Urusi kufanya mashambulio katika mji mkuu wa Ukraine, Kiev. Ripota huyo Vira Hyrych aliuawa baada ya nyumba yake  kupigwa na kombora. Urusi ilifanya mashambulo hayo  wakati katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres alipokuwa anafayna ziara kwenye mji wa Kiev.

Soma:Milipuko katikati mwa mji wa Kyiv huku Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa akifanya ziara nchini Ukraine.

Nembo ya Shirika la kutetea haki za binadamu la Human Rights Watch
Nembo ya Shirika la kutetea haki za binadamu la Human Rights WatchPicha: John MacDougall/AFP/Getty Images

Wakati huo huo shirika la kutetea haki za binadamu la Human Rights Watch limeitaka Poland itekeleze wajibu wa kuwalinda wakimbizi wa Ukraine waliomo nchini  humo. Shirika hilo limeitaka Poland itimize wajibu wake kwa kuwapatia watu hao makaazi, usafiri na ajira za uhakika. Kwa mujibu wa taarifa ya asasi hiyo, haki za baadhi ya wakimbizi wa Ukraine zinakiukwa nchini Poland. Kulingana na takwimu za walinzi wa mpakani wakimbizi wa Ukraine zaidi ya milioni 3 wameshaingia nchini Poland tangu majeshi ya Urusi yaivamie Ukraine mnamo mwezi Februari.

VyanzoDPA/https://p.dw.com/p/4AawA