Ujerumani yasherehekea miaka 20 ya kuungana
3 Oktoba 2010BERLIN
Sherehe zimeanza nchini Ujerumani kuadhimisha miaka 20 tangu pale Ujerumani Magharibi na Mashariki zilipoungana, ambapo kutakuwa na sherehe katika mitaa mbali mbali pamoja na matamasha ya muziki katika mji mkuu Berlin, Bremen na kwingineko. Tarehe 3 Oktoba , 1990 Ujerumani iliungana baada ya kutengana kwa miongo minne . Ukuta wa Berlin ulianguka kiasi miezi 11 kabla wakati Wajerumani waliposherehekea muungano wao mbele ya bunge mjini Berlin. Tangu wakati huo, Oktoba 3 ni siku ya mapumziko . Mwaka huu mji wa Bremen ndio umepewa hadhi ya kuanda rasmi sherehe hizo. Maafisa wa mji huo walitengeneza mfano wa Ukuta wa Berlin, kama kumbukumbu ya historia ya ukuta huo ulivyotenganisha Ujerumani mbili. Kansela Angela Merkel anasubiriwa kutoa hotuba baadaye leo mjini Bremen.