1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani yakaribia kufuzu michuano ya Euro 2020

Bruce Amani
14 Oktoba 2019

Ujerumani inayoendelea kujijenga imepiga hatua zaidi kuelekea katika mashindano ya Ulaya mwaka ujao lakini kazi bado ipo ya kukigeuza kizazi cha sasa cha wachezaji chipukizi na kuwafanya kuwa washindani.

https://p.dw.com/p/3RG5z
EM-Quali Deutschland - Estland
Picha: Reuters/I. Kalnins

Majeruhi, maradhi, vituko vya mitandao ya kijamii vilikigubika kipindi hiki cha michuano ya kimataifa lakini mwisho wa siku kitu kimoja kilichokuwa muhimu ni kuwa vijana hao wa kocha Joachim Loew wanakaribia michuano ya Euro 2020.

Ushindi wa 3 – 0 dhidi ya Estonia jana, kufuatia sare ya 2 – 2 na Argentina, umeiweka Ujerumani kwenye mkondo wa kufika mashindano ya Euro yatakayoandaliwa katika nchi tofauti. Huyu hapa kocha Joachim Loew akiuzungumzia mchezo wa jana

Ikiwa utacheza kwa muda mrefu ukiwa pungufu uwanjani, nadhani kwa dakika 80, basi ni vigumu hata dhidi ya waestonia. Katika kipindi cha kwanza ilibidi tujipange upya na bila shaka tukawa na matatizo kadhaa, lakini katika kipindi cha pili, timu ilicheza vyema sana kwa kuudhibiti mpira na hivyo mabao yakapatikana.

Nahocha wa kikosi hicho Manuel Neuer alizungumzia umuhimu wa kuwa na kikosi cha wachezaji wapya huku akiyasifia mabadiliko anayoyafanya kocha Loew

Ni mabadiliko. Mimi ndiye mwenye umri mkubwa Zaidi katika timu zote. Nina miaka 33.inafurahisha sana kuwajua vijana hawa, kizazi kipya. Pia inatia moyo sana kuona jinsi watakavyocheza na bila shaka kama mchezaji mwenye uzoefu, unajaribu kusaidia na kuwaonyesha namna ya kuwajibika uwanjani. Hilo ni muhimu sana kwao. Lakini woite ni wachezaji mahiri, wenye motisha na uchu. Na hilo ni muhimu sana, kuwa na uchu wa mafanikio.

Uholanzi inaongoza Kundi C mbele ya Ujeurmani ijapokuwa timu zote mbili zina pointi 15 kila moja. Ireland Kaskazini wako nyuma na pengo la pointi tatu lakini watawaalika Waholanzi na kisha kumalizia Ujerumani kumaanisha kuwa nafasi zote za kufuzu bado zipo wazi. Ujerumani watawaalika Belarus November 16 wakati Uholanzi ikikamilisha mechi zake dhidi ya Estonia siku tatu baadaye.