1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani yaipa Tanzania msaada wa euro milioni 70

Florence Majani26 Oktoba 2021

Katika kuadhimisha miaka 60 ya mahusiano kati ya Ujerumani na Tanzania, serikali ya Ujerumani imetoa kiasi cha Euro milioni 71 kwa serikali ya Tanzania fedha zitakazotumika katika shughuli mbalimbali za maendeleo. Florence Majani anaripoti kamili.

https://p.dw.com/p/42BfA

Ingawa hii si mara ya kwanza kwa Ujerumani kutoa msaada wa kifedha kwa Ujerumani, lakini msaada huu uliokabidhiwa Jumatatu ni mahsusi kabisa katika kuadhimisha miongo sita ya mahusiano mema bainaya pande hizi mbili.

Balozi wa Ujerumani Tanzania, Regina Hess, amesema fedha hizi zitakatumika katika afya, maji na udumishaji wa haki za wanawake na watoto.

"Tumefurahi kufanikisha majadiliano haya ya miradi ya Maendeleo na fedha hizi zitatumika katika maeneo manne la kwanza ni Afya, maji, uimarishaji wa sekta ya fedha na uchumi  na utunzaji wa mazingira," amesema Regina Hess.

Balozi Regina amesema hii ni mara ya kwanza kwa Tanzania kuingia makubaliano hayo tangu mwaka 2015 kutokana na changamoto kadhaa ikiwamo Covid-19.

Balozi wa Ujerumani nchini Tanzania Regine Hess
Balozi wa Ujerumani nchini Tanzania Regine HessPicha: DW/H. Bihoga

Balozi huyo amesema ushirikiano baina ya Tanzania ulianza mwaka 1961 mara tu baada ya uhuru wa Tanganyika.

Ushirikiano huu upo katika maeneo mengi, ikiwamo sanaa na utamaduni, ulinzi na hata Masuala ya elimu.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango, Amina Shabani amesema ushirikiano huo ni wa muhimu na msaada wa euro milioni 71 ambazo ni sawa na shilingi bilioni 45, milioni 466, laki 783 kwa fedha za Kitanzania utatumika kupunguza umaskini katika maeneo muhimu ya kimaendeleo ikiwamo utawala bora na usimamizi wa fedha.

Hafla ya utiaji saini ushirikiano huo ilihudhhuriwa pia na Balozi wa Marekani Tanzania, Donald Wright, na Wawakilishi wa sekta mbalimbali za maendeleo hapa nchini Tanzania.