1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani yabanduliwa katika hatua ya makundi

2 Desemba 2022

Ujerumani imebanduliwa katika michuano ya Kombe la Dunia katika hatua ya makundi kwa mara ya pili mfululizo licha ya ushindi wa mabao 4-2 dhidi ya Costa Rica.

https://p.dw.com/p/4KN05
WM 2022 Deutschland Costa Rica Niederlage
Picha: Martin Meissner/AP Photo

Washindi hao mara nne wa Kombe la Dunia waliingia uwanjani wakihitaji ushindi lakini pia walikuwa wakitegemea matokeo ya mchezo kati ya Japan na Uhispania ili kufuzu kwa raundi ya mchujo ya 16 bora.

soma Qatar 2022: Argentina, Poland na Australia nazo zafuzu kwa duru ya 16 bora

Hata hivyo ujerumani iliondolewa katika Kundi E kutokana na tofauti ya mabao huku Japan ikipata ushindi tena baada ya kuilaza Ujerumani katika mechi nyengine ya matokeo ya kushtua kwa kuifunga Uhispania 2-1.

Ujerumani walichukua uongozi wa mapema lakini mambo yalibadilika katika kipindi cha pili huku kocha Hansi Flick akifanya mabadiliko mengi, akijibu matokeo ya moja kwa moja ya mechi kati ya Japan na Uhispania.

soma pia Kombe la Dunia: Brazil na Ureno zafuzu duru ya mtoano

Kutangulia sio kufika

Fußball WM Katar | Costa Rica v Deutschland
Picha: Hassan Ammar/AP/picture alliance

Kikosi cha Ujerumani kilianza vyema na kuiadhibu Costa Rica kupitia mchezaji Serge Gnabry aliyepachika wavuni bao kwa kichwa baada ya kuunganisha mpira wa krosi kutoka kwa beki wa Leipzig David Raum kunako dakika ya 10 ya mchezo.

Dakika saba tu baada ya kipindi cha pili kuanza, taarifa zilitanda kwenye Uwanja mkubwa wa Lusail kwamba Japan walikuwa wamefunga mabao mawili ya haraka na kuongoza dhidi ya Uhispania, matokeo ambayo yangeilazimisha Ujerumani kuondoka kwenye dimba hilo.

Flick alijibu mara moja, akimleta Niclas Fuellkrug na kumtoa kiungo Ilkay Gundogan. Kunako dakika ya 58 ya mchezo Costa Rica walitumia fursa na kupachika bao la kwanza kupitia mchezaji Yeltsin Tejeda, na dakika ya 70 mlinda lango Manuel Neur alifanya makosa katika lango lake na kujifunga mwenyewe.

Ujerumani ilijibu tena kupitia mchezaji Kai Havertz na kunako dakika ya 86 Fuelkrug alipachika la 4na mechi hiyo kukamilika kwa 4-2.

Uhispania yaponea

FIFA World Cup Qatar 2022 - Group E - Spain v Costa Rica
Picha: DYLAN MARTINEZ/REUTERS

Licha ya Uhispania kufungwa 2-1 na Japan imefuzu kwa raundi ya mchujo wakiwa na pointi 4 sawa na Ujerumani tofauti ya wingi wa mabao waliyovuna katika mechi yao ya ufunguzi dhidi ya Costa Rica walipoipa kipigo cha mabao 7-0.

Ubelgiji vile vile waliondolewa katika michuano ya kombe la dunia baada ya sare ya 0-0 na Croatia, ambayo ilisonga mbele kama timu iliyoshika nafasi ya pili katika Kundi F nyuma ya Morocco.

soma Kombe la Dunia 2022: Senegal imekuwa nchi ya kwanza ya Afrika kuvuka ngazi ya makundi

Dakika chache baada ya mchezo huo, kocha wa Ubelgiji Roberto Martinez alitangaza kujiuzulu jukumu lake baada ya zaidi ya miaka sita.

Romelu Lukaku, anarekodi nzuri ya ufungaji kwa Ubelgiji lakini amerejea hivi karibuni baada ya kuuza jeraha aliingia kama mchezaji mbadala wa wakati wa mapumziko lakini alipoteza nafasi, bora zaidi kufika dakika za lala salama baada ya kushindwa kupachika wavuni krosi kutoka kwa Thorgan Hazard.

Croatia, mshindi wa pili wa mwaka 2018 , itajitahidi kupambana tena kama ilivyofanya katika Kombe la Dunia la mwaka 1998 baada ya kufika pia nusu fainali.

 

AFP/AP