1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani na Afrika kuimarisha ajira kwa vijana wa Afrika

John Juma
28 Novemba 2017

Serikali ya shirikisho la Ujerumani imejitolea kuunga mkono Umoja wa Afrika katika juhudi zake za kutoa mafunzo na ajira kwa vijana, na kwamba wametenga Euro milioni 28 kuimarisha maarifa barani Afrika

https://p.dw.com/p/2oP5V
EU Afrika Gipfel Merkel 02.04.2014 Brüssel
Picha: Reuters

Afrika ndilo bara lenye idadi ya watu wenye umri mdogo zaidi duniani. Watu hao wanaweza kuleta mabadiliko ya kuboresha mustakabali wa Afrika ikiwa watapewa nafasi muhimu. Hayo yamesemwa na mwakilishi maalum wa kansela wa Ujerumani barani Afrika Guenter Nooke, katika mkesha wa mkutano wa kilele wa Umoja wa Ulaya na Afrimka mjini Abdijan.

Kwenye mkutano wake na naibu mwenyekiti wa Muungano wa Afrika Kwesi Quartey, na mwenyekiti wa Biashara Afrika Albert Yuma, pembezoni mwa mkutano wa kilele wa Umoja wa Ulaya na Afrika unaoanza kesho mjini Abidjan Cote d`Ivoire, mwakilishi huyo maalum wa Kansela wa Ujerumani Guenter Nooke, amesema serikali ya shirikisho la Ujerumani, imejitolea kuunga mkono Umoja wa Afrika katika juhudi zake za kutoa mafunzo na ajira kwa vijana, na kwamba wametenga Euro milioni 28 kuimarisha maarifa barani Afrika na Euro milioni 3 kwa utekelezwaji wa sera ya uhamiaji ambayo pia inahusiana na ajira na uhamiaji.

Mpango wa kukuza maarifa Afrika

Mkutano wa kilele wa Mungano wa Ulaya na Afrika mwaka 2017 unalenga kuimarisha sekta ya ajira kwa vijana
Mkutano wa kilele wa Mungano wa Ulaya na Afrika mwaka 2017 unalenga kuimarisha sekta ya ajira kwa vijanaPicha: picture-alliance/dpa

Mpango wa maarifa kwa Afrika ambao unatekelezwa na ushirikiano mpya wa shirika la Maendeleo ya Afrika NEPAD, ni hazina wazi. Taasisi zinazotoa mafunzo ya kiufundi, sekta za binafsi katika kanda ya TVET na washirika wengine katika baadhi ya nchi za Afrika wanaweza kuomba ufadhili, kuboresha vituo vyao na kuimarisha mafunzo au kuanzisha mtaala mpya miongoni mwa mambo kadhaa.

Nooke alipongeza juhudi za sekta binafsi katika kuimarisha mafunzo kwa vijana. Amesema "kwa ushirikiano wa sekta binafsi na mafunzo, kuna hakikisho kuwa vijana wanapata maarifa yanayokwenda sambamba na mahitaji ya masoko. Hali hii inaboresha nafasi za mtu kuajiriwa kazi na kupata kazi nzuri. Ameongeza kuwa ipo haja kulenga zaidi sekta binafsi barani Afrika wala si tu ile ya serikali.

Haja ya kubadilisha mifumo ya elimu Afrika

Naibu mwenyekiti wa Umoja wa Afrika Kwesi Quartey amewasilisha pongezi za halmashauri kuu ya Umoja huo kwa serikali ya Ujerumani kwa ushirikiano wa muda mrefu na kwa msaada wake. Ameeleza kuwa lengo la mwaka huu la kubuni nafasi zaidi za ajira kwa kuboresha maarifa ya vijana kiufundi na kibiashara ni muafaka na linkwenda sambamba na kauli mbiu ya Umoja wa Afrika ya mwaka huu. Ameongeza kuwa kile ambacho bara la Afrika linalazimika kulifanaya ni kutathmini upya mifumo yake ya elimu na lipanue viwango vya maarifa ili viwe sawa na mahitaji. La sivyo ukuaji katika sekta za viwanda, uzalishaji na maendeleo yatasalia kudumaa ikiwa vijana hawataandaliwa vyema kwa ajira.

Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron na rais wa Burkina Faso Christian Kabore wakikagua gwaride la heshima mjini Ouagadougou
Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron na rais wa Burkina Faso Christian Kabore wakikagua gwaride la heshima mjini OuagadougouPicha: Getty Images/AFP/L. Marin

Balozi Georg Schmidt ambaye ni mkurugenzi katika wizara ya mambo ya kigeni ya serikali ya Ujerumani ametilia mkazo mada ya vijana  kwamba haihusu tu ajira. Amesema vita vinapotokea, vijana ambao huathirika mno hulazimika kupigana au huwa waathirikaa wa machafuko, na kwamba wapo vijana wengi wanaokabiliwa na mzongo wa mawazo kwa sababu ya machafuko. Kwa sababu hiyo, Ujerumani itazidi kuunga mkono juhudi za amani na udhibiti katika bara Afrika kwa ushirikiano wa karibu na Umoja wa Afrika na mashirika ya kikanda. Pande zote zimetoa hakikisho kuwa zitaendelea kushirikiana katika siku zijazo

Macron: "Simo miongoni mwa wanaoiambia Afrika kitu cha kufanya"

Katika tukio jingine, rais wa Ufaransa Emmanuel Macron amesema kuwa hatoki katika kundi la viongozi watakaoiambia Afrika kitu cha kufanya, bali ataelekeza juhudi zake kuinganisha Afrika na Ulaya. Amesema hayo wakati wa hotuba yake kwa wanafunzi wa chuo kikuu mjini Ouagadougou Burkina Faso. Ameongeza kuwa hatasimama pamoja na wale wanaosema Afrika inazongwa na shida na migogoro, bali atakuwa miongoni mwa wale wanaoamini bara la Afrika halijapotea  na wala halihitaji kuokolewa

Macron yupo katika ziara ya siku tatu Magharibi mwa Afrika ambapo pia atahudhuria mkutano wa kilele wa Umoja wa Ulaya na Umoja wa Afrika mjini Abidjan utakaohudhuriwa  pia  na Kansela Angela Merkel wa Ujerumani

Mwandishi: John Juma/RTRE/PR- FRG Embassy (Addis Ababa )

Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman